Thursday, 28 August 2014

MTAANI KWETU



        VALANGATI KIVULINI

Ndugu zangu leo Kivulini kwetu kumetokea valangati la kufa mtu.



Majira kama ya saa tano asubuhi maeneo ya mtaa wa madukani niliukuta umati wa watu wakishuhudia patashika nguo kuchanika baina ya akinamama wawili. Vurugu iliyokuwapo pale ilikuwa si ya kuzimwa na wapita njia. Mungu ashukuliwe baada ya msukosuko mkubwa kwa bahati wakapita askari wa Tigo na pikipiki lao ndio waliofanikiwa kumaliza kasheshe ile tena baada ya kulipua kabomu kadogo ka kutoa machozi.



Utulivu uliporejea nikapata fulsa ya kuongea na mmoja wa mashuhuda waliokuwepo kutoka mwanzo ili nijue chanzo cha kadhia hiyo; ndipo nilipopewa mkanda mzima.



Chanzo chetu cha habari kinasema kisa cha ugomvi huo ni mwekezaji wa ndani ambaye ana hotelibaa pale mtaani palipotokea ugomvi. Inasemekana mwekezaji huyo alikuwa amemwajiri dada mmoja kutoa huduma katika mradi huo ambaye kutokana na umahiri wake na bidii yake ya kazi akaamua kumuongeza jukumu la kumhudumia pia yeye mwekezaji binafsi.



Chanzo chetu cha habari kinaendelea kumwaga cheche kwa kusema kuwa baada ya kipindi kifupi tokea mwekezaji huyo amtunukie shahada mhudumu wake akatokea mteja mmoja wa kike ambaye naye kutokana na umaarufu wake katika ile hotelibaa ikapelekea mwekezaji kumtunukia medali ya uteja wa kutukuka na hivyo mbali ya kuwa mteja katika mradi akawa pia mteja wake binafsi.



Changanya kanganya hii iliendelea kwa kipindi cha kama mwezi mmoja hivi bila mteja bora na mhudumu mahiri kutambuana kuwa wapo katika kujenga nyumba moja. Wenyewe wakawa wanacheka na kuchangamkiana sana kiasi cha kuwa mashosti. Lakini wapo baadhi ya wateja na wahudumu katika kiwekezwa hicho ambao walikuwa wanajua kuwa urafiki huo ulikuwa ni wa mashaka; kwamba walikuwa wakila sahani  moja bila wenyewe kugusana mikono.



Kikichotokea leo ni kama ajali. Ilikuwa ni kawaida kwa mwekezaji kumpa kinoti kama kibali mteja bora kumpelekea mhudumu mahiri  ili apewe huduma aliyokuwa anaitaka na pesa atalipa atakapojisikia. Kwa bahati mbaya leo aliandika vinoti viwili; kimoja cha huduma kwa mteja na kingine cha huduma kwa mwekezaji; vikiwa katika karatasi zinazofanana. Kwa uzembe wa mteja bora alipofika kwa shosti wake akajichanganya na kutoa kinoti cha huduma binafsi ya mwekezaji ambamo ndani ya kinoti hicho kulikuwa na jina la mteja bora lililoanza na haneeilikifuatiwa na saa ya kukutana, mahali pa kukutana, nini cha kufanya na mambo mengine ambayo hayaandikiki na chini ya kinoti hicho kulitiwa saini kwa mbwembwe na mwekezaji mwenyewe.

Mhudumu mahiri baada ya kupokea kinoti hicho kwa makosa na yeye akakosea kumhoji kwa kumuuliza mteja bora ana maana gani kumpatia ujumbe ambao si wake ama ndiyo kantangaze anaianzia kwake. Mteja bila kengere kogonga kichwani kwake akahoji kuwa kama ujumbe haumuhusu maneno yote hayo yanakujaje; kwani inahuu..



Majibizano yakiwa katika hatua za awali, mara akaingia mwekezaji pale hotelibaa; kuingia kwake ikawa kama unazima moto kwa kupulizia gesi asilia. Yakaanza kurushwa maneno, jembe, matusi, vitisho, kutoka pembe hadi pembe; aliyekuwa na masikio ya chuma alisikiliza na mwenye masikio ya mbao alisalimisha masikio yake maana  matusi na kashfa zilizokuwa zikimwagwa pale zilikuwa ni mpya kutoka  dukani ambazo zilikuwa hazijawahi kutumika. Kana kwamba hiyo haitoshi vitendea kazi na bidhaa zikaanza kutumika kama silaha za mapambano na ukumbi wote wa biashara ukawa mbengelembengele; vurumai hadi barabarani. Ilibidi ili kujenga heshima mwekezaji aingie mitini na kuacha gari liende bila dereva maana mambo sasa yalikuwa si mambo.



Baada ya kupata taarifa hiyo nikabaki ninajiuliza kufanya vurugu kiasi hiki wale akina dada mashosti wakati wote ni madoezi maana yake nini na yule mwenye mali aliyeko nyumbani afanyeje ? Na huyu mwekezaji naye huu ndio kweli utaratibu wa kuwekeza; kwa kuwa na mhudumu mpaka binafsi na mteja mpaka binafsi. Kwa staili hii uchumi kivulini kwetu utaimarika kweli ?

No comments:

Post a Comment