Wednesday, 1 April 2015

CHONDE CHONDE SIMU ZITATUPELEKA PABAYA

Kwa kipindi kirefu Kivulini kwetu tulikuwa tunasikia tu kuwa kuna ugonjwa umeingia nchini unaitwa UBISI. Mara ya kwanza kuusikia tulidhani jina limekosewa; kwamba badala ya "ubishi" wameuita "ubisi"; lakini baada ya kuhoji mara mbili mbili tukahakikishiwa kuwa hilo jina la UBISI ni sahihi; kwamba ni kifupisho cha maneno Ulevi Binafsi wa Simu.


Awali tuliuposikia ukitajwa tukajua kuwa hayo ni mambo ya mjini; uzushi, soga, hadithi, mipasho n.k.
Lakini jana kwa mara ya kwanza tulijionea mwenyewe kile ambacho awali tulikipuuza, kuwa nchi imeingiliwa na ugonjwa wa Ubisi.

 Tulikuwa tumepanda gari kutoka Makumbusho kwenda Posta. Kama bahati tulikaa kiti cha nyuma. Tulipofika mataa ya Morocco tukastaajabu kidogo kutokana na ukimya uliokuwepo kwenye gari; tukataka kujua kulikoni;tusije tukawa tumepanda gari la kwenda kwenye msiba. Tulichokiona ndicho kilichotusukuma kuyasema haya; kwamba kumbe karibu robo tatu ya abilia walikuwa wamezama kwenye simu zao. Hata kondakta wa basi ilibidi afanye kazi ya ziada kupata nauli yake; watu na simu, simu na watu.

Tulipofika Posta kama kawaida yetu tukaanzisha mjadala wa wazi juu ya ugunjwa huu wa Ubisi; hapo ndipo tulipohakikishiwa kuwa hivi sasa Simu ni janga la Taifa.


Katika mjadala huo usio rasmi tukabaini mambo mengi sana. Wapo waliosema kuwa Ubisi umevunja ndoa nyingi sana nchini. Wengine wakasema Ubisi umefelisha wanafunzi wengi sana vyuoni. Hapohapo tukaambiwa mbali na ubisi kufukuzisha watu kazi; kwa waliobaki kazini umechangia kushusha viwango vyao vya utendaji kazi. Walinzi wamevamiwa malindoni kutokana na ubisi. Hospitali wagonjwa wamesababishiwa vifo kutokana na ubisi wa madokta na manesi. Familia zimelishwa vyakula  vibichi au vilivyoungulia sababu ya ubisi. Waumini hawasikilizi mahubiri makanisani na misikitini kutokana na ubisi. Makaburini kwenye mazishi ubisi unatuandama. Watoto hawalelewi vizuri sababu ya ubisi wa mama zao na walezi wao. Magari yamepata ajali na watu kuumia au kufa shauri ya ubisi wa madereva. Biashara zimedorora kutokana na ubisi. Nidhamu imeshuka sana kila sehemu kutokana na ubisi. Pesa inaskwisha kutokana na ubisi.


Kutokana na hili sisi Kivulini kwetu tukadhani japo tumechelewa kidogo tuwashike bega ndugu zetu, jamaa zetu na rafiki zetu kuwa tujiangalie na huu ulevi binafsi wa simu. Sasa hivi simu  zimetutawala kiasi kwamba tumejisahau na kusahau wajibu wetu. Toka asubuhi watu tumo katarazaji kutoka Facebook kwenda Twitter; kutoka twitter kwenda instagram; kutoka instagram kwenda WhatApp; kutoka WhatsApp kwenda Viber; kutoka Viber kwenda Tango; kutoka Tango kwenda immo; kutoka immo kuingia google; kutoka google kuibukia kwenye mablog, website na takataka kibao. Na mtu akizama hapo hata umwite vipi hakusikii labda umpige kibao. Hakika huu ugonjwa ni hatari sana japo ni wa kujitakia.


 Na ili uende sambamba nao ni lazima uwe na simu zaidi ya moja na uhakika wa muda wa maongezi. Hutaijua hasara ya simu mpaka uwe mkweli katika kufuatilia kiasi cha pesa kinachotumika kwa ajili ya muda wa maongezi; hufikia kwa wengine simu zao kutumia mara mbili zaidi yao wao binafsi. Ubisi unatupeleka puta.


Pamoja na kuwa simu si anasa; bado nina hofu na matumizi yetu ya simu kama kweli yana tija yoyote katika maisha yetu. Wengi wetu simu zinatuharibia maisha.



Ombi langu kwenu jamaa zangu kila mtu kwa wakati wake ajitolee kuchangia vita vya ubisi kwa kupunguza japo saa moja ya matumizi yake ya kila siku ya simu. Kumbukeni hapo nimeelezea hasara zake kiuchumi tu sijagusia masuala ya mionzi n.k. Naomba kutoa hoja. 


No comments:

Post a Comment