Sunday, 5 April 2015

TABIA MBAYA ZA WAHUDUMU WA BAR NA HOTELI

Kama mjuavyo leo ni sikukuu ya Pasaka. Pamoja na kuwa si maadili lakini hiyo ndiyo hali halisi ilivyokuwa; Kivulini kwetu na sisi tuliamua kutoka kwenda maeneo kusafisha macho. Hatukwenda wote sehemu moja bali tulitawanyika maeneo mbalimbali kwa maelekezo kwamba ifikapo muda tuwe tumerejea kujumuika pamoja kama familia kupata kilichoandaliwa kwa ajili ya siku ya leo.

Kivulini kwetu kutokana na utaratibu wa kuongozwa na nidhamu, ulipotimu muda kila mmoja wetu alifika nyumbani mapema. Kwa kuwa tulikuwa tumewahi ilibidi kusubiri kidogo maandalizi yakae sawa tupate kuendelea na kipindi hicho. Wakati tukisubiri ilianzishwa mada ambayo kutokana na umuhimu wake tusingelipenda kuwanyima ndugu zetu uhondo; na pengine kupata maoni juu ya namna ya kukomesha tabia hizi za hawa ndugu zetu wahudumu.

 Image result for wahudumu wa bar



Mmoja wetu kutokana na alichokiona alisema wahudumu hawa na hasa wa kike wana tabia mbaya sana ya kuwaombaomba wateja wawanunulie soda, bia ama chakula. Inasemekana huwa nawaoni haya wala vibaya kumwomba mteja hata kama hiyo ni mara ya kwanza wameonana nae. Kwa namna wanavyoomba humfanya mteja akereke kiasi kwamba hata akimpa huwa anampa kwa shingo upande ili kuondoa hiyo kero ili aendelee na starehe zake bila ya bugudha yoyote.

 Image result for wahudumu wa bar

Kituko kingine cha hawa wahudumu ni uzito wa kurejesha chenji na hata wakirejesha huwa siyo kamili kwa kisingizio cha chenji kuwa tatizo. Penye 800/= ukitoa noti ya sh. 1000/= usitarajie kuipata 200/=; penye 4000/= au 4500/= ukitoa noti ya sh. 5000/= usutarajie kuipata sh. 1000/= au 500/= na ukiipata ni sharti ugombane. Hii ni kwa upande wa chenji; lakini pia kuna mchezo wa kuongezeana bei; chakula cha 2500/= utatajiwa sh. 3500/=, ama chakula cha 4000/= utaambiwa sh. 4500/= au 5000/= ili mradi kipatikane kiasi chochote mbali na kiasi stahiki wakichukue kama chao. Kazi kubwa huwapata wale ambao huwa wamelewa kidogo ama wanaoonekana wana pesa nyingi na hawapendi kulumbana au kuonyesha wana gubu kwa kudaidai chenji.

Tatizo jingine lililobainishwa kwa ndugu hawa ni udoezi. Wapo wahudumu hasa akina dada ambao hudiriki kwenda kunawa maji kabisa na kuja kuketi mezani kwa wateja na kuanza kula nao vipande vya kuku na mishikaki bila ya hata kukaribishwa kwa kisingizio cha kuonja kama vimeiva au chumvi imekolea; pengine husingizia kuwasindikiza wateja kimaongezi. Wapo ambao huchukua glasi na kumimina soda ya mteja au bia na kunywa. Ukiwaona unaweza kudhani ni wacheshi kwa wateja kumbe ni wadoezi wakubwa.

Tuliambiwa kwamba wapo wahudumu visirani ambao hupenda kuwahudumia wateja wanaokuja peke yao tu na pindi wajapo na wenza wao huwa ni wazito kutoa huduma na watoapo huwa wanenuna ama hutoa huduma mbaya kwa makusudi. Ukiagiza bia baridi utaletewa ya moto, ukiagiza supu ya kuku utaletewa ya mbuzi na wakati mwingine unaweza kuambia kitu fulani hakipo kumbe kipo; wao huwa ni vituko kwa kwenda mbele ili mradi siku nyingine usirudie tena kuja sehemu hiyo na huyo uliyeongozana naye.

Wapo wahudumu ambao wakikuzoea sana huwa hawana adabu wala heshima; anaweza kusema chochote na popote bila kujali uko katika mazingira gani ama uko na nani. Aweza kukwambia amekumiss sana wakati hana uhusiano na wewe; aweza kuanza kukuuliza hali ya mkeo au mmeo wakati hamjui; aweza kukucheka kuwa umefulia kwa sababu leo unakunywa soda badala ya bia; anaweza kukwita shemeji kwa sababu tu jana alikuona umekaa na rafiki yake. Wabaya zaidi ni wale ambao hupita wakitangaza kuwa mteja fulani ni mtu wake na kutoa onyo kwa wenzie wasimhudumie isipokuwa yeye; na wakati mwingine hutwangana makonde kumgombania mtu ambaye hana habari nao kabisa; kisa ni kuwa mteja anaonekana anazo. Utashangaa kama una mazoea na sehemu siku unakwenda unaona kila mhudumu anaogopa kukusogelea kutokana na vitisho wakati mteja mhusika hujui kinachoendelea.

Kero jingine ni wahudumu  ambao huja kazini na kutumia muda wao mwingi kuchezea simu na kusoma magazeti ama kuongea na washikaji wao na kuacha kuwahudumia wateja. Mteja anaweza kukaa zaidi ya dakika kumi bila ya kuulizwa ahudumuwe nini na wakati huohuo kuna wahudumu kibao wamezagaa na kila mmoja anafanya lake ambalo ni nje ya majukumu yake ya kazi. Na akitokea mteja kujaribu kulalamika; majibu atakayopata hatodiriki kurejea tena mahali pale.

Kivulini kwetu baada ya kupata aina hizi za wahudumu tulijaribu kujiuliza kuwa ni nini chanzo cha matatizo hayo. Tulichogundua ni sababu kadhaa ambazo tunadhani zikifanyiwa kazi matatizo haya ya huduma za hoteli na bar yatapungua kama siyo kwisha kabisa.

Tulibaini kuwa sababu ya kwanza ni kuwa wahudumu wengi hawakusomea kazi hizo na wala kupigwa japo msasa wakati wanapatiwa ajira hizo hivyo hawana kabisa elimu yoyote juu ya wanachotakiwa kukifanya; na kuna wengine ambao huwa hata darasa la saba hawakumaliza. Tunadhani wakati umefika wa wenye mahoteli na bar kuajiri wahudumu waliopitia mafunzo ili huduma zikidorora tujue ni sababu nyingine na si ya elimu au mafunzo.

Tulibaini pia kuwa hawa wahudumu wengi hulipwa mshahara mdogo sana usiotosheleza hata nauli ya kuja kazini kwa wiki mbili na pamoja na kuwa mshahara ni mdogo huwa hawapewi wote kwa pamoja na bado kiasi kikubwa hukatwa kwa kisingizio cha kuvunja chupa, glasi n.k. ama kupata shoti katika malipo ya huduma; hivyo ili waweze kumudu maisha inabidi wawe ombaomba kwa wateja wao kufidia upotevu ama kupata cha kurudi nacho nyumbani kwa matumizi yao. Wengine inasemekana hupatiwa nafasi ya kuhudumia lakini bure kwa makubaliano kuwa atumie uwepo wake mahali hapo kupata pesa ya kujikimu; vipi atapata hiyo huwa ni akili kichwani mwake. Tunadhani waajiri wa wahudumu hawa wawe waungwana kwa kuwalipa kwa mujibu wa sheria na kanuni kwani maisha ni magumu na hali ni ngumu sana ya maisha; kumtumikisha mtu bila ya kumlipa sio uungwana hata kidogo.

Tuligundua pia kuwa wahudumu hawa huajiriwa kwa kufuata sura zao na maumbile yao kuwavutia wateja na wala si uwezo wao wa kazi ama wito wa kazi. Na mbaya zaidi hulazimika kutoa rushwa ya ngono kwa wamiliki wa mahoteli ama mameneja wahoteli na bar hizo. Hivyo huwa na kiburi toka siku ya kwanza kwa kuamini hata akifanya madudu tayari alikwisha hakikishiwa usalama wa ajira yake na mwenye mali au meneja. Wenye hoteli na bar wakumbuke hawa ni wahudumu wa watu na wanastahili kuheshimu na kuheshimiwa; kuajiri mtu kama kitu ni kuleta kero mahali pa kazi na mwisho wa siku hata biashara hudumaa kutokana na wateja kuacha kuja mahali hapo.

Kitu kingine tulichokibaini ni kuwa wahudumu hawa wengi wao wamepambana na misukosuko ya maisha mapema kabla ya umri wao. Wapo waliopewa mimba na kukimbiwa; kati yao wapo waliozaa na wengine kutoa mimba. Wapo waliofukuzwa au kutengwa na familia zao kwa sababu mbalimbali . Wapo waliokimbia ndoa zao. Wapo waliokimbia masomo n.k. Kutokana na sababu hizo wengi wao wana hasira na maisha na wanatembea na nadhiri kuwa siku wakipata mwanya wakufanya lolote kulipiza kisasi wanaweza kufanya. Wanaweza kumwibia tajiri, wanaweza kumuibia mteja, wanaweza kumchoma mtu kisu n.k. Hali hii hufanya maeneo ya hoteli na bar kuwa kichaka cha kuficha kundi la watu wenye hasira na walipa visasi ambao kila mtu mbele yao humwona adui. Matajiri wawe makini katika kuajiri kwa kujaribu japo kupata historia za wafanyakazi wao ili kuwa na uhakika wa usalama mahala pao pa kazi.

Kuvilini kwetu inaamini sana katika huduma bora kwa mteja na haki kwa wafanyakazi; na ili kwenda sawa ni vema kufuata taratibu na sheria katika ajira za wahudumu.




No comments:

Post a Comment