MGENI KUTOKA MAJUU
Jana
tumepata bahati ya kutembelewa na mgeni kutoka ng’ambo. Mgeni huyu aliwasiri
kivulini kwetu akiwa na maoni kadhaa kwenye mkoba wake kama zawadi badala ya vitu ambavyo
tumevizoea kuletewa na wageni wa aina hii.
Kwanza
mgeni huyu alitupongeza kwa kuunda chombo cha mawasiliano cha kisasa(blog)
kwa madai kuwa angalau tunaonyesha upeo fulani wa maendeleo kwa kwenda na
wakati.
Akiwa
kivulini kwetu alituomba tuendeleze mawasiliano na watu wa mataifa mbalimbali kutumia blog
hiyo kwani dunia ya leo ni kama kijiji; na tujitahidi kuweka mambo ya msingi badala ya kuijaza matusi na uchafu
kama zilivyo blog nyingine nyingi.
Baada
ya kutuasa hivyo alitupatia ujumbe toka umoja wa mabloga wa kwao kuwa sisi wa
kivulini kwa faida yetu na ya vitukuu wetu tuzingatie yafuatayo:
1.
Tujitahidi kuanzia sasa kupunguza kasi ya kuzaliana; tusisubiri maji yakiwa
shingoni ndipo tuweke sheria kalikali. Amedai kuwa ardhi hii tunayoiona kubwa
haitakuwa hivi baada ya miaka kumi ijayo kama matumizi yenyewe yatakuwa kwa
kufuja kama ilivyo sasa. Kingine kitakachotuumbua ni huduma za jamii; kwamba
wao kwao pamoja na maendeleo waliyonayo katika aina mbalibali ya huduma za majii bado kuzaa zaidi ya watoto wawili
katika familia ni kama ajali; labda mama ajaliwe kujifungua mapacha watatu.
Tukumbuke watoto wazaliwapo wanahitaji chakula, matibabu, nguo, elimu na mambo
mengi sana hivyo kuzaa bila mpango si busara. Kila mwanakivuli atoe busati, badala yake aweke nyota ya
kijani mlangoni kwake.
2.
Tupunguze siasa tufanye kazi. Ameshangazwa sana alipowasili kivulini na kumkuta kila mwanakivuli ni
mwanasiasa, mwanaharakati na mwanasheria. Alishangaa kuona kivuli duni kama chetu kina wanaharakati wengi kushinda wataalam wa fani mbalimbali. Ameshangaa kuona tunapoteza muda mwingi sana
kuongea, kushitakiana, kubishana, kulaumiana, na kujadiliana mambo mengi sana ambayo wala hayana tija wala
umuhimu; tena tunayafanya tukiwa katika makundi huku tukimwaga mapesa mengi kupata muafaka . Yeye alisema ipo haja ikibidi tupange siku maalum
za longolongo ziwe japo siku mbili kwa wiki
na siku tano zilizobaki kusiwe na vikao, mikutano, vijiwe wala mabonanza
tujikite katika kazi. Yeye amedai kuwa hakuna kokote walikopata maendeleo kwa
maneno bali kwa kazi. Ametishika sana kukuta robo ya wanakivuli ndio wanaofanya
kazi na robo tatu yote ni wategemezi. Tumesahau hata msemo mtakatifu usemao "ASIYEFANYA KAZI NA ASILE".
3.
Tatu, alitusihi kuwa wazalendo. Ameshangaa kutuona watu wa kivulini
pamoja na matatizo yetu hatujipendi wenyewe na baya zaidi hatupendani. Alishangaa sana kumsikia kijana
wetu mmoja tena msomi aliyesomeshwa na serikali akitamka hadharani bila kujali kazungukwa na nani anasema kwamba anajuta kuzaliwa
kivulini; eti ni heri angelizaliwa mbwa
majuu angeliishi kwa raha sana. Anadai tamko la aina hii kule kwao mtu huyu
angelipigwa risasi kwani hana faida na tena ni sumu katika jamii. Kama ni kwenye kompyuta hiki kingelikuwa kirusi hatari sana. Amedai kuwa
bila ya uzalendo sera nzuri, katiba bora na mipango mizuri havitaweza kutusadia
chochote. Ni lazima turingie kivuli chetu.
4.
Jambo jingine; alitusihi watu wa kivulini tuwe waadirifu
na hasa viongozi. Ameshangaa jinsi ambavyo hatushangai wala kuhoji maajabu ya
kiuchumi yaliyopo kivulini. Kwamba tumeamua kutohoji chochote wala kuwianisha kazi ya mtu na
kipato chake. Kwamba si ajabu tarishi wa mahakama kumiliki gari ya vogi.
Haitushangazi mtoto wa kazi kuwa na jumba la kifahari kijijini kwao. Ni kitu
cha kawaida waziri kumiliki ardhi ya wilaya nzima kwa ajili ya kilimo cha
familia yake. Mwanafunzi kumiliki simu ya milioni na zaidi ni kawaida. Amedai
kwa mwendo huu tuna kama miaka mitano tu iliyobaki maisha kivulini
yasiwezekane. Kundi la walionacho limezidi kuwa dogo mno likiishi katika msongo wa maisha magumu yasiyo na matumaini hata chembe; wakati huohuo kuna kundi dogo linaloishi kama liko mbunguni; linaishi kadri linavyowaza. Amedai kuwa hii
inaongeza chuki na hasira za kundi kubwa; na inavyoonekana muda si mrefu
uvumlivu wa wengi utatoweka watajichukulia vyao walivyoporwa na wachache.
5.
Mgeni huyu amewasilisha mshangao kutoka majuu kuwa kivulini mungu
katujalia kwa kutupa kila kitu ambacho wenzetu wamepewa kimoja kimoja au viwili
ama hawakupata kabisa. Kasema tumepewa bahari, mito, maziwa, wanyama, ardhi,
madini, maajabu, na vingine vingi. Anadai bado anatafiti kuona wapi lilipo
tatizo kiasi cha sisi kushindwa kuongoza kwa utajiri duniani. Amediriki hata
kusema kuwa pengine mataifa kakubwa yanatufanyia chumaulete kutuibia uchumi
wetu kwa mazingira ama tumepigwa kipapai au tumekanyaga mdudu. Amedai lazima rasilimali zetu zitunufaishe wenyewe kwanza sio tunagawa kama njugu ili mradi tu ziishe.
6.
Mwisho ametuonya tusichezee amani tuliyonayo. Ameshauri kila mwenye
kuleta chokochoko tumpe skolashipu aende kusoma digrii ya amani Somalia, Misri,
Parestina au Zaire ili akirejea
afundishe wengine. Amesema maeneo hayo kuna vyuo vizuri sana vya amani; hivyo ni vema vijana wetu tuwaendeleze katika fani hiyo pia.
Baada ya kutupa salamu hizo akatukabidhi zawadi ya
msalaba mwekundu akaondoka.
No comments:
Post a Comment