Friday, 22 August 2014

MGENI NJOO MWENYEJI APONE


         MGENI KUTOKA MAJUU


Jana tumepata bahati ya kutembelewa na mgeni kutoka ng’ambo. Mgeni huyu aliwasiri kivulini kwetu akiwa na maoni kadhaa kwenye mkoba wake  kama zawadi badala ya vitu ambavyo tumevizoea kuletewa na wageni wa aina hii.




Kwanza mgeni huyu alitupongeza kwa kuunda chombo cha mawasiliano cha kisasa(blog) kwa madai kuwa angalau tunaonyesha upeo fulani wa maendeleo kwa kwenda na wakati.



Akiwa kivulini kwetu alituomba tuendeleze mawasiliano na watu wa mataifa mbalimbali kutumia blog hiyo kwani dunia ya leo ni kama kijiji; na tujitahidi kuweka mambo ya msingi badala ya kuijaza matusi na uchafu kama zilivyo blog nyingine nyingi.



Baada ya kutuasa hivyo alitupatia ujumbe toka umoja wa mabloga wa kwao kuwa sisi wa kivulini kwa faida yetu na ya vitukuu wetu tuzingatie yafuatayo:



1.      Tujitahidi kuanzia sasa kupunguza kasi ya kuzaliana; tusisubiri maji yakiwa shingoni ndipo tuweke sheria kalikali. Amedai kuwa ardhi hii tunayoiona kubwa haitakuwa hivi baada ya miaka kumi ijayo kama matumizi yenyewe yatakuwa kwa kufuja kama ilivyo sasa. Kingine kitakachotuumbua ni huduma za jamii; kwamba wao kwao pamoja na maendeleo waliyonayo  katika aina mbalibali ya huduma za majii bado kuzaa zaidi ya watoto wawili katika familia ni kama ajali; labda mama ajaliwe kujifungua mapacha watatu. Tukumbuke watoto wazaliwapo wanahitaji chakula, matibabu, nguo, elimu na mambo mengi sana hivyo kuzaa bila mpango si busara. Kila mwanakivuli atoe busati, badala yake aweke nyota ya kijani mlangoni kwake.


2.      Tupunguze siasa  tufanye kazi. Ameshangazwa sana alipowasili kivulini na kumkuta kila mwanakivuli ni mwanasiasa, mwanaharakati na mwanasheria. Alishangaa kuona kivuli duni kama chetu kina wanaharakati wengi kushinda wataalam wa fani mbalimbali.  Ameshangaa kuona tunapoteza muda mwingi sana kuongea, kushitakiana, kubishana, kulaumiana,  na kujadiliana mambo mengi sana ambayo wala hayana tija wala umuhimu; tena tunayafanya tukiwa katika makundi huku tukimwaga mapesa mengi kupata muafaka  .  Yeye alisema ipo haja ikibidi tupange siku maalum za longolongo ziwe japo siku  mbili kwa wiki na siku tano zilizobaki kusiwe na vikao, mikutano, vijiwe wala mabonanza tujikite katika kazi. Yeye amedai kuwa hakuna kokote walikopata maendeleo kwa maneno bali kwa kazi. Ametishika sana kukuta robo ya wanakivuli ndio wanaofanya kazi na robo tatu yote ni wategemezi. Tumesahau hata msemo mtakatifu usemao "ASIYEFANYA KAZI NA ASILE". 



3.      Tatu, alitusihi kuwa wazalendo. Ameshangaa kutuona watu wa kivulini pamoja na matatizo yetu hatujipendi wenyewe na baya zaidi hatupendani.  Alishangaa sana kumsikia kijana wetu mmoja tena msomi aliyesomeshwa na serikali akitamka hadharani bila kujali  kazungukwa na nani  anasema kwamba anajuta kuzaliwa kivulini;  eti ni heri angelizaliwa mbwa majuu angeliishi kwa raha sana. Anadai tamko la aina hii kule kwao mtu huyu angelipigwa risasi kwani hana faida na tena ni sumu katika jamii. Kama ni kwenye kompyuta hiki kingelikuwa kirusi hatari sana. Amedai kuwa bila ya uzalendo sera nzuri, katiba bora na mipango mizuri havitaweza kutusadia chochote. Ni lazima turingie kivuli chetu.



4.      Jambo jingine;  alitusihi watu wa kivulini tuwe waadirifu na hasa viongozi. Ameshangaa jinsi ambavyo hatushangai wala kuhoji maajabu ya kiuchumi yaliyopo kivulini. Kwamba tumeamua kutohoji chochote wala kuwianisha kazi ya mtu na kipato chake. Kwamba si ajabu tarishi wa mahakama kumiliki gari ya vogi. Haitushangazi mtoto wa kazi kuwa na jumba la kifahari kijijini kwao. Ni kitu cha kawaida waziri kumiliki ardhi ya wilaya nzima kwa ajili ya kilimo cha familia yake. Mwanafunzi kumiliki simu ya milioni na zaidi ni kawaida. Amedai kwa mwendo huu tuna kama miaka mitano tu iliyobaki maisha kivulini yasiwezekane. Kundi la walionacho limezidi kuwa dogo mno likiishi katika msongo wa maisha magumu yasiyo na matumaini hata chembe; wakati huohuo kuna kundi dogo linaloishi kama liko mbunguni; linaishi kadri linavyowaza. Amedai kuwa hii inaongeza chuki na hasira za kundi kubwa; na inavyoonekana muda si mrefu uvumlivu wa wengi utatoweka watajichukulia vyao walivyoporwa na wachache. 



5.      Mgeni huyu amewasilisha mshangao kutoka majuu kuwa kivulini mungu katujalia kwa kutupa kila kitu ambacho wenzetu wamepewa kimoja kimoja au viwili ama hawakupata kabisa. Kasema tumepewa bahari, mito, maziwa, wanyama, ardhi, madini, maajabu, na vingine vingi. Anadai bado anatafiti kuona wapi lilipo tatizo kiasi cha sisi kushindwa kuongoza kwa utajiri duniani. Amediriki hata kusema kuwa pengine mataifa kakubwa yanatufanyia chumaulete kutuibia uchumi wetu kwa mazingira ama tumepigwa kipapai au tumekanyaga mdudu. Amedai lazima rasilimali zetu zitunufaishe wenyewe kwanza sio tunagawa kama njugu ili mradi tu ziishe.



6.      Mwisho ametuonya tusichezee amani tuliyonayo. Ameshauri kila mwenye kuleta chokochoko tumpe skolashipu aende kusoma digrii ya amani Somalia, Misri, Parestina au Zaire ili  akirejea afundishe wengine. Amesema maeneo hayo kuna vyuo vizuri sana vya amani; hivyo ni vema vijana wetu tuwaendeleze katika fani hiyo pia.



Baada ya kutupa salamu hizo akatukabidhi zawadi ya msalaba mwekundu akaondoka.

No comments:

Post a Comment