BONANZA KIVULINI
Jana Kivulini kulikuwa na Bonanza. Wenyewe wanasema hilo
Bonanza ni tamasha la aina yake ambalo hujumuisha burudani na michezo ya aina
mbalimbali. Kama mjuavyo hayo ni moja ya marupurupu ya kuwa na amani nchini. Watafiti wanadai kuwa
huwezi kukuta mabonanza kwa Waparestina
na wengine ambao kila uchao huna uhakika kama kesho utakuwepo.
Tamasha hilo kwa kweli lilifana sana. Vijana waliitikia
vilivyo wakacheza, wakala mpaka wakanywa.
Kilichoninikwaza mimi,na pengine na wenzangu wengi ni
matumizi mabaya ya bonanza hilo, hasa kwa upande wa vijana. Nilishangazwa sana
kuona namna walivyokuja kivulini bila ya kujistiri maungo yao; hususani akina
dada. Wengi walikuja wamevaa vipande vya nguo na kuacha sehemu muhimu za maungo
yao bila ya kufunikwa.Mungu bariki kumbe vijana wa siku hizi si wakware wala wabakaji.
Labda unaweza kusema nguo za michezo
ndivyo zilivyo. Lakini si hivyo. Mimi jezi nazijua. Zile hazikuwa jezi bali ni
nguo zao za nyumbani. Sikuweza kuelewa vizuri kama hivyo walivyokuja kivulini
ndivyo walivyotoka majumbani kwao ama la. Lakini kubwa ni swali ambalo
nilijiuliza mpaka leo sijapata jibu kuwa akina dada hawa kutujia vile walikuwa
wanataka tuelewe vipi ama walikusudia kutuonyesha nini ? Ninachelea kusema hata
vipande hivyo walivyovaa walikuwa wakiogopa Dola; vinginevyo wanavyoonekana
wangelikuja kama walivyozaliwa kwani walikuwa wamebakiza padogo sana.
Na akina kaka nao sikuwaelewa. Wengi walivalia sarawali zao
nusu ya vikalio na kuacha ngua zao za ndani zikionekana. Kana kwamba hilo
halitoshi wengi walikuwa wametengeneza nywele na kuvaa vidani kiasi kwamba
ilikuwa wakati mwingine vigumu kumtofautisha mtu na dada yake. Hawa nao
walikuwa na ajenda gani kutufanyia vile ?
Yawezekana mwanakivuli mimi nimepitwa na wakati. Na iwe
hivyo; ila kusema kweli vijana hawa ni wazi nao wamepitiwa na wakati; wakati
unawaburuta mzobemzobe kuwapeleka ambako wala hawakujui. Hivi kwa utaratibu huo
wa kuparaganya maumbile, si tunazikonyeza Sodoma na Gomora nyingine ?
Wazazi wapendwa, waalimu, wanazuoni, na viongozi wa dini ebu
saidieni kizazi hiki; sijui kama wanaharakati na hili mnahusika au nyinyi ni
katika siasa, katiba na sera za serikali. Tusaidiane katika kazi hii nzito.
Kwa ushahidi zaidi nawaalikeni wote mje katika Bonanza
kivulini tarehe kama ya jana kuanzia saa 12 asubuhi hadi saa moja usiku katika
viwanja vyetu vilevile mje mjionee vimbwanga vya dijitali.
No comments:
Post a Comment