Thursday, 5 March 2015

SAFARI YA KUTOKA UZALENDO WA KAWAIDA KWENDA UASI KUPITIA UZALENDO CHOTARA

 Leo Kivulini kwetu tunakuja na kilio kingine ili tuungane na Watanzania wenzetu wenye mawazo kama yetu kukataa na kuchukua hatua kabla hatuhafika mbali.

Kilio chetu ni juu ya zile harakati za kutusafirisha bila ya ridhaa yetu kutoka kwenye Uzalendo halisi wa nchi yetu kutupeleka kwenye Uzalendo Mwitu au Uasi kwa jina jingine dhidi ya nchi yetu.

Japo tumechelewa kutafakari lakini ni heri tumejitahidi kuliwaza hilo wakati tayari tumekwisha fikishwa katika Uzalendo Chotara.

Wataalamu wanasema siku zote ukiweka viumbe wawili wenye asili moja iwe ni mmea au mnyama na wakakaa kwa kipindi fulani, cha kwanza kutokea huwa ni kiumbe chotara na baadae kiumbe cha asili mojawapo.




Tunaamini kuwa yeyote anayejichanganya kimaongezi mitaani na katika mitandao atakubaliana na sisi kuwa kauli, mawazo na mtizamo wa wananchi wengi kwa sasa unaashiria ukomavu wa Uzalendo Chotara; yaani mawazo na mtizamo wa wananchi kutoridhishwa na mwenendo mzima wa nchi yao, wananchi kutowapenda viongozi wao, wananchi kulalamikia karibu kila jambo, Uzalendo wa kubeza, kukejeri, na kulaani kila jambo. Kauli za utengano, kauli za dharau,  na kauli za vitisho. Kuna kauli nyingi sana ambazo hatukuzoea kuzisikia katika nchi yetu sasa hivi zimekuwa ni za hawaida; watu hawaoni haya wala hawaoni vibaya.

Kivulini kwetu tumebaini kuwa kustawi kwa uzalendo huu chotara hakukuja kama ajali; tunaamini kabisa uzalendo huu ulitokana na mchanganyiko wa Uzalendo halisi na Uzalendo mwitu. Watu waliudaka Uzalendo mwitu katika upya wake wakidhani kuwa huo ndio ustaarabu. Kwamba ili uonekane msomi mzuri basi uwe na kifua cha kuisema serikali na kukashifu nchi; kwamba ili uonekane tajiri basi shurti uwakashifu wananchi na uwakejeri viongozi; kwamba ili uonekane umetembea sana duniani, basi uweze kuponda mambo ya kwetu na kuimba mambo ya ughaibuni; kwamba ili uonekane mtu makini ni lazima uchote fedha za umma na uhujumu nchi;  Tuliingia mkenge kupitia utandawazi tukajiona tumepata na kumbe tumepatikana.

Hapo mwanzo ilikuwa ni aibu mtu kusimama na kujidai kuwa ana shamba ekari 2000 Mpanda;  au ana maroli 90 ya kusafirisha mafuta ama ana vijisenti kama dola 20 milioni Uswisi  kwani ni kiasi ambacho kilikuwa kikivuta hisia ya utovu wa Uzalendo. Sasa hivi hata wanafunzi wanaweza kuwa na mali; nani atawauliza ? Nakumbuka enzi ya Sokoine mtu kuonekana na bidhaa kiasi fulani; haikuwa na haja ya mamlaka kumfuatilia bali yeye mwenyewe kwa jinsi alivyolelewa alikuwa anaona aibu. Waswahili wana sema kawaida ni kama sheria. Watu kama Sokoine hawakumbukwi kwa ukorofi wala sura zao bali wanakumbvukwa kwa Uzalendo wao.

Tumefika mahali ambapo Uzalendo Chotara huo unaanza kututafuna. Tulianza kwa kulia kizaire kwa kutumia magitaa sasa hivi tunalazimika kulia kwa midomo na machozi machoni. Tumechoka na mvurugano wa mawazo, tumechoshwa na msongamano wa itikadi na tumechanganyikiwa na hekaheka za falsafa  kila uchao. Tunaamini yapo mazuri na tunaamini pia yapo mabaya lakini kuyapambanua inatupa shida kutokana na kupigiwa makelele kila uchao na magwiji wa Uzalendo Mwitu. Sasa hivi wao ndio wanaojua kila kitu na wanatulazimisha na sisi tufanye watakavyo. Haiwezekani.

Tunadhani ni wakati muafaka kuelezana haya ili kukusanya nguvu tuweze kuachana na safari hii mbaya. Ikiwa hapa tu katikati tulipofika hali imekuwa mbaya kiasi hiki je tukizidi kuendelea huko itakuwaje ? Tunadhani ule Uzalendo tuliouacha nyuma ndio mali kuliko huo Uzalendo Mwitu tunaoufuata. Kama maendeleo ndiyo haya ni heri turudi nyuma kwani hata tukiyapata maendeleo hayo hayatusaidii; sana sana yatatuacha tukiwa mahututi na taabani.

No comments:

Post a Comment