EBU FIKIRIA WEWE UNGELIKUWA ALBINO UNGEJISIKIAJE
Ndani ya hotuba hiyo kulikuwa na mambo kadhaa ambayo singelipenda nirarejee ila miongoni mwayo lilikuwepo suala ya Mauaji ya Albino(Ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi). Sipendi nirejee alichosema ila ningelipenda niliongee kwa namna nyingine; nia ikiwa ni kujaribu kuwasaidia wale ambao pengine hawakuweza kuelewa nini kilichokuwa kikisisitizwa katika hotuba ya Rais.
Nadhani wote tunakubali kuwa hayupo aliyebahatika kutoa maoni ama mapendekezo azaliwe vipi; hivi tulivyozaliwa tulijikuta tumezaliwa hivyo. Wapo watu ambao wangelipenda wazaliwe wanawake lakini kwa mapenzi yake mola wamejikuta wamezaliwa wanaume. Na wako wanaume ambao wangelipenda wazaliwe wanawake lakini bahati haikuwa yao badala yake wamezaliwa wanaume. Ni kwa mifano hiyo walioutaka ufupi wakapewa urefu, walioutaka weupe wakapewa weusi na kadharika na waliotaka wazaliwe kawaida wakazaliwa Albino. Na ndiyo sababu kila uchao binadamu hujifanyia marekebisho katika kazi ambayo mwenyezi mungu aliifanya bila ridhaa yake ili angalau kuifurahisha nafsi yake. Tumeshuhudia wanaume wakisuka nywele na kuvaa bangili na mikufu ili angalau wafanane na wanawake; tumeshuhudia akina mama wakijichubua kutoa rangi nyeusi wawe weupe na kuvaa nywele za singa wawe kama wazungu au waarabu; tumeshuhudia wafupi wakivaa viatu vya mchuchumio waonekane angalau warefu kidogo; tumeshuhudia wembamba wakinywa dawa za "kichina" wawe wanene; na mengine mengi. Lakini katika madawa yote sijaisikia dawa ya kumfanya Albino awe na ngozi ya kawaida; pengine wangeliweza kubadili ngozi zao ili kujisalimisha na wauaji hawa.
Kwa kuwa hayupo hata Albino mmoja aliyeomba azaliwe hivyo bali wamezaliwa kwa mapenzi yake mola. Mimi au wewe tungweliweza kuzaliwa Albino kwa sababu tunajua hatukushiriki kujichagulia rangi ya kuzaliwa nayo. Sasa kwa ukweli huo hii jeuri ya kwanza kuwanyanyapaa Albino inatoka wapi na hii imani ya kuwa Albino wanavuta mafanikio inatoka wapi. Rais kauliza jana kuwa kama imani hiyo ina ukweli wowote kwanini basi hao Albino wakiwa mwili kamili hawakuwa mamilionea ila wakiwa vipandevipande wanaleta utajiri ?
Na iwe iwavyo, ni binadamu gani ambaye leo akiambiwa kuwa apoteze maisha yake ili japo watoto wake wapate utajiri atakuwa tayari; na hilo linakuwaje jepesi kwa wenzetu ?
Utaratibu wa kuwavamia na kuwacharanga kinyama Albino ni unyama ambao hauna lugha nzuri ya kuuelezea ukaeleweka katika uzito wake. Kwanza hawa wenzetu wanao upungufu katika kuzaliwa; kana kwamba hilo halitoshi tunawaongezea janga jingine la kuwaua; hii ni laana ambayo kama hatukuifanyia kazi italiangamiza taifa letu. Tunajisikiaje kusoma habari zao magazetini, kuziona katika TV; kwamba leo mmoja kacharangwa kule, kesho mwingine kauawa huku na tunatikisa miguu kana kwamba tunaangalia mechi ya Simba na Yanga ama Filamu ya King Majuto; hatuoni haya wala hatusikii vibaya. Ipo sinema moja ilikuwa ikionyesha ukatili huo wanaofanyiwa Albino; binasfi sikuweza kuiangalia hadi kufika robo; inatisha.
Ebu kila mtu ajifikilie na yeye angelikuwa Albino; anasikia habari za Albino wenzake wanavyouawa; na yeye anakuwa akitembea akijua wakati wowote atavamiwa na kunyofolewa kiungo chochote; hajui aende wapi akajifiche na kwa nini afanye hivyo; ana makosa gani katika dunia hii. Jamani tumwogope mungu. Kama hiyo ndiyo namna ya kutajirika ebu tufikirie namna nyingine; vinginevyo tukubali kubaki maskini kuliko kuwa matajiri juu ya damu za watu tena watu wenyewe walemavu wa ngozi. Ukiendesha gari la kifahari, ukienda kutalii Dubai, ukila kuku, ukinywa bia; mwenyewe unajisifu kuwa imetokana na mkono au mguu wa Albino. Kama ndivyo wewe ni shetani aliye hai ambaye huna haki na kuchanganyika na binadamu wa kawaida. Na ulaaniwe ufe mapema tena ufe kinywa kikiwa wazi kama ishara ya ubaya ulioutenda duniani kwa hao watakaoihudumia maiti yako.
Kitaifa hii ni vita; na iwe vita ya kila mmoja wetu kuhakikisha kila fununu juu ya vitendo hivi inafanyiwa kazi. Walio karibu na waganguzi wawe makini nao na wazifuatilie nyenendo zao ili kuweza kubaini kama wanahusika na chochote juu ya mauaji haya. Ma Albino tuwalinde popote walipo; tusiwatenge bali tuambatane nao ili angalau wapate imani kuwa jamii ipo nao. EBU KILA MMOJA WETU AFIKIRIE KAMA ANGELIKUWA ALBINO KWA MAISHA HAYA ANGELIJISIKIAJE.
No comments:
Post a Comment