SIMU KUTOKA KWA MGOMBEA MTARAJIWA
"Halo ndugu zangu Kivulini,
Muda wowote kuanzia sasa Chama chetu kitaanza mchakato wa kutuchuja. Wakati tukisubiri muda huo ufike nilitaka niwatoe hofu wapenzi wangu wote kuwa uwezekano wa mimi kuwemo katika kumi bora hauna shaka kabisa.........tano bora pia sina wasiwasi..............kidooogo nina mashaka na tatu bora; japo hapo napo endapo sifa zitazingatiwa ipasavyo naweza kuvuka.
Moyo wangu unanidunda sana katika kuteuliwa kuwa mgombea pekee wa nafasi hiyo muhimu.
Kitu kingine ambacho ningependa kuwapa kama akiba ni kuwa mmoja kati ya jamaa zangu endapo nitaingia nae katika tatu bora nina uhakika kabisa na nafasi ya ugombea mwenza.
Baada ya kuwapa matumaini hayo ningelipenda kuwafahamisha kwamba nitakuwa radhi na matokeo yoyote ili mradi rafiki zangu wawili hawatakuwemo katika tano bora. Nasema hivyo kutokana na harakati zao ambazo kwa kiasi kikubwa kiliathiri sana mchakato huu kwa wagombea wengi tangu utangazaji nia, uchukuaji fomu mpaka urejeshaji fomu kiasi kwamba sina imani na hata mienendo yao hapa mjini katika kipindi hiki kigumu cha subra.
Kitu ambacho ninawapasha wana Kivulini kwetu na wapiga kura wote ni kuwa jiandaeni safari hii kushuhudia maajabu katika uteuzi kwani hautakuwa ndani ya matarajio yenu mlio wengi. Matokeo ya uteuzi yatawaacheni midomo wazi. Cha msingi wote mtafurahia uteuzi huo ambao hautarajiwi.
Mimi japo sijitaji ni miongoni mwa hao ambao wapo nje kabisa ya mawazo yenu na nina matumaini makubwa kabisa ya kuwa mgombea mtarajiwa. Hata hao watakaoingia tatu bora mtashangaa na roho zenu.
Ili nisije nikasema na kupitiliza naomba niishie hapa nikiwaomba ndugu na rafiki zangu mniombee niteuliwe kwani mimi ndiye nitakayekuwa mkombozi wenu pekee miongoni mwa wagombea wote.
Ahsanteni sana kwa kunisikiliza."
Tulidhani ni vizuri tukawaonyesha wote ujumbe huu ambao ni kama utabiri wa aina yake ambao pengine utaweka vizuri kisaikolojia wale ambao kwa muda sasa tumekuwa tukijiapiza kuwa matokeo yatakuwa yale tunayoyawaza sisi.