Wednesday, 17 December 2014

GUBU

     GUBU LILIVYO



Kuna tabia ambayo watu wengi wanayo; tabia ambayo bila ya wao kujua huwa inawakera wengine na kuwakwaza vilevile. Tabia hii ni ya Gubu.


Mtu mwenye gubu anakera sana kwani daima huwa hana jambo dogo kwake; kila jambo liwe la maana ama la kipuuzi ataliongea kwa muda mrefu na mara kwa mara kiasi kwamba msikilizaji unaweza kuamua kumtoroka  kwa kuchoshwa na kuongelea jambo hilo hilo kwa muda mrefu.


Mtu mwenye gubu daima huwa ni mlalamishi, hashauriki, hajui kusamehe na baya zaidi huwa hakubali makosa. Yeye daima hujiona ndiye anayestahili na kwamba yeye ndiye huwa benki ya matatizo.


Mtu mwenye gubu neno lake halisahauliki; aliliongea jana, leo analiongea na kesho lazima ataliongelea.


Mtu mwenye gubu mada zake hazibadiliki; kama ni sera za chama, mambo ya mpira, au matukio ya jamii; basi kila anayekutana naye. bila kutafakari kuwa anapendelea jambo hilo au hapendelei; yeye ataanza kufunguka. Na haishii hapo atasogea pengine, napo ataendelea na jambo lilelile.


Mtu mwenye gubu huwa hampendi kabisa mtu asiyemsikiliza aongeapo mambo yake, humpenda sana anayemuunga mkono na kumshangilia hata kama anaongea utumbo.


Mtu mwenye gubu daima ni mtu wa visasi, vitisho na mbwembwe nyingi sana; usipomjua unaweza kuingia mkenge ukadhani hakuna mwingine zaidi yake.

Monday, 13 October 2014

HARAKATI VICHWANI MWETU TUMEWACHOKA

ACHENI KUTUSINGIZIA

Kivulini kwetu jana tulikutana kujadiliana juu ya upuuzi huu ambao umekuwa kila siku ukifanywa na wanasiasa uchwara na wanaharakati njaa kuwa  kila waliwazalo wao hushindwa kuliwasilisha kama mawazo yao na kusingizia kuwa ni matakwa ama mawazo ya wananchi.

Nasema tulijadili kwa pamoja tukaamua kutoa tamko kuwa tuwapashe na kuwaeleza wazi kuwa waache kabisa kama sio kukoma kudumisha harakati zao juu ya vichwa vyetu.

Kwa hali ilivyo sasa jamaa hawa ni vema wakajua kuwa kuna kila fulsa na kila nyenzo za kumwezesha kila mwananchi kuwasilisha mawazo yake popote na wakati wowote juu ya nini anawaza, nini anahitaji na kipi hakitaki. wananchi wa sasa wamesoma na wana upeo wa kufikiri na uwezo mkubwa wa kuzungumza. Wananchi wa sasa si watu wa kusemewa na si mbumbumbu kiasi cha kila siku kusingiziwa kuwa wanataka hili ama wanataka lile. Kama wazo lako ni jema au zuri kwanini usiliseme kama wewe na badala yake unatafuta uzito kwa kusingizia kuwa ni wazo la wananchi, walikutuma lini ?

Inaudhi sana kumkuta mtu mzima na masharubu yake kasimama jukwaani anatoka mapovu akijidai anawasilisha maoni ya wananchi; yeye kama nani awasemee watu na anaowasemea wako wapi. Na katika udhaifu, na uvumilivu walionao wananchi hawamkemei wala kumzomea; wanamsikiliza kwa matumaini kuwa pengine atakuwa na jipya la kuwaeleza; mpaka muda unakwisha wanabaini kuwa alichongea ni pumba tupu toka mwanzo hadi mwisho.

Mwanzoni baadhi ya majimbo tulikuwa tukiwasilishiwa mawazo yetu na wabunge bungeni; imefikia sasa mbunge wengi hakanyagi kabisa majimboni na wala hawana mawasiliano na wapiga kura wao, lakini mbunge huyohuyo akifika bungeni anaongea kama kasuku mambo na mawazo aliyoongea na mkewe kwa kuyafanya ndiyo mawazo ya wananchi;  toka lini mke wako akawa ndiyo wananchi. Acheni mambo yenu.

Ukitaka jaribu kuyafuatilia anayoyasema; utakuta ni mambo tofauti ya jinsi ilivyo katika jimbo lake. Kwa wale ambao wanawasiliana na wapiga kura wao ni sahihi kuwasemea kwani walitumwa; lakini hao wengine ambao nawasema leo ambao siku hadi siku wanaongezeka idadi kwa kweli ni kero tupu na wanayatia aibu majimbo yao.

Na hao ambao kila uchao huitisha mikutano na waandishi wa habari wakidai wanatoa hoja za wananchi ama wanadai haki za wananchi, hivi ni wapi wanakaa na wananchi tunawaeleza kuwa hivyo ndivyo tunavyotaka. Utasikia wananchi hawataki hiki ama wanataka kile; cha ajabu haohao tena wanadai kuwa tutawahamasisha wananchi wasikubali ama wakubali; kama ni kweli wanachosema ni mawazo yetu iweje waje tena kutuhamasisha tukubali ama tukatae; si watuache tu tutakubali au kukataa wenyewe kwa wakati wetu; waokoe muda wautumie kulea watoto wao. Kinachoonekana sasa ni watu kutumia vyama na taasisi kuomba chochote kwa wajomba zao kwa kusingizia kuwa wanakuja kutusaidia wananchi kumbe wezi wakubwa. Tumewachoka wezi hawa na ipo siku tutawapiga mawe wakija kivulini kwetu. Harakati hizo na siasa hizo tumezichoka. Mambo ya kujenga magorofa juu ya vichwa vyetu tumeyastukia; kila siku nyinyi tu ndio mnaojua mawazo yetu nyie mawazo yenu anayajua nani; ebu oneni haya msidhani hatujui ujanja wenu na vitaasisi vyenu feki.

Tuesday, 7 October 2014



            SUALA LA UCHAFU

Kivulini kwetu safari hii tunataka kuongelea suala la uchafu katika mji wetu. Suala hili limekuwa kama tabia na inaelekea tabia hii inaimarika sana na kuwa utamaduni wa jamii yetu.
Kama tujuavyo uchafu ni takataka; lakini pia uchafu ni hali ya kutokuwa msafi. Uchafu pia inaweza kuwa tabia ya mtu au watu kutokuwa wasafi.
Wakati tukitathmini uchafu kuna namna nyingi ya mtu au watu kutokuwa wasafi.
Namna ya kwanza ambayo ni rahisi kuelezeka ni tabia ya watu kutoona kinyaa kukaa katika mazingira yenye takataka kama vile masalia ya matunda, matambara, makaratasi na kadharika. Lakini pia kukaa mahali penye uvundo ama panapotiririka maji machafu, kwenye mifereji michafu na kadharika.


Uchafu mwingine ni tabia ya kutotunza mazingira kwa kutupa taka ovyo, kula ovyo, kuvaa ovyo na kadharika.


Uchafu mwingine ni kutokuwa na mpangilio mzuri wa vitu hata kama vitu hivyo ni visafi. Mfano katika mji ni kuegesha magari ovyo, kupanga bidhaa ovyo hadi barabarani, ujenzi holela, migongamano isiyo ya lazima, kufanya shughuli zozote mahali pasipostahili kama kupika sehemu za wazi, kulala kwenye mavaranda, kuosha magari barabarani, gereji kwenye makazi ya watu, vituo vya mafuta kwenye makazi ya watu, viwanda vya jua kali mahali pasipostahili na mengine mengi ya aina hiyo

.
Baada ya kufuatilia kwa karibu tumegundua kuwa chanzo cha hali hii ni mamlaka husika za mji kutowajibika katika kusimamia sheria na taratibu za mji. Aidha si kutosimamia tu bali kutokuwa na mipango au utaratibu endelevu katika kuuweka mji namna unavyopasa kuwa.


Mamlaka zimeshindwa kutoka maelekezo fasaha na kwa wakati juu ya kipi kifanyike, wapi kifanyike, nani afanye na afanye wakati gani. Na juu ya hayo kueleza wazi kuwa atakayekiuka maelekezo hayoatafanywa nini na kweli inapotokea mtu kakiuka basi hatua zichukuliwe.


Kinachojitokeza ni kusimamia machache baadhi na kusimamia kwake ni kinyume na inavyotakiwa; kwamba upo upendeleo kwa baadhi ya watu, kwa baadhi ya maeneo na baadhi tu na masuala yote yanayotakiwa kusimamiwa. Matokeo ya kufanya hivi ni jamii nzima kuachwa njiapanda watu wasijue ni kipi sahihi kufanyika na nani anapaswa kufanya kwani katika eneo moja, watu wa aina moja, katika muda unaofanana; wapo wanaoruhusiwa kufanya na wapo wanaozuiwa kufanya kitu kilekile, mahali palepale na katika muda uleule.


Chanzo kingine cha uchafu ni tabia ya mtu mmoja mmoja ya uchafu. Hii inatokana aidha na malezi, ukosefu wa elimu, umaskini na mlengo wa kushoto wa mawazo.


Kitendo cha mtu kula matunda na kutupa maganda barabarani, kitendo cha mtu kunywa maji au soda na kutupa chupa katika mfereji, tabia ya mtu kuuza bidhaa zake dukani na makasha, maboksi, na vifungio vingine ovyo mbele ya duka lake, vitendo vya watu kujisaidia haja kuwa na ndogo katika mifereji ya majitaka wakati mwingine mchana kweupe, vitendo vya kupanga bidhaa za chakula juu ya maji yanayotiririka na kuwauzia watu na hata wao pia kununua; lakini mbaya zaidi kitendo cha kuona haya yote yanafanyika na kuacha kuyakemea; yate haya yanajumuika katika tabia ya uchafu. Watu wamekuwa hawaoni vibaya juu ya masuala haya na imekuwa ni kawaida.


 Hujitokeza kuacha kwa muda pindi wanapotangaziwa na mamlaka waache kutokana pengine na milipuko ya magonjwa ama kuwe na ugeni unakuja Kivulini kwetu. Katika harakati hizo za kuzuia uchafu watu hulalamika sana kuwa wanaonewa na kunyanyaswa katika nchi yao kwa kuambiwa waachane na uchafu. Baada ya milipuko na ugeni kuondoka hali ya uchafu hurejea mahali pake. Kwa hakika inasikitisha sana.


Binafsi nilidhani ipo haja kwanza ya jamii ambamo na wenye mamlaka wanatoka humo ibadilike na kuchukia mazingira machafu. Tuwe jamii yenye kuona kinyaa  kukaa kwenye majalala, kutupa taka ovyo, kujisaidia ovyoovyo, kununua vitu vichafu, kuvaa mavazi machafu, sisi wenyewe kutokuwa wachafu; kwa sababu nakumbuka kuna siku alipanda mtu mmoja kwenye daladala(simtaji jina, siitaji jinsia yake, dini yake wala kabila japo niliulizia na vyote nikaambiwa) kila abiria ilibidi afunge pua; lakini hiyo haikutosha wakaomba mtu huyo ashushwe vinginevyo wao washuke; ikabidi ashushwe kituo kinachofuata; kwani kwa jinsi alivyokuwa ananuka ni afadhari ya kinyesi; unaweza kupata hiyo picha kuwa mtu huyu anatoka wapi na amewakera watu kiasi gani katika maeneo yote aliyopita. Mtu kama huyu kuna uchafu gani utakaomtisha akaogopa ?


Lakini juu ya jamii kujirekebisha, mamlaka nazo ziweke utaratibu mzuri wa kufuatwa. Kuwe na sheria za kufuatwa ili kuweka mji katika usafi. Taratibu zizuie baadhi ya mambo yanayosababisha uchafu kufanyika na taratibu hizo zisimamiwe bila ya ubaguzi wala upendeleo na usimamizi huo uwe endelevu na sio zima moto.
Ninasali ije itokee kipindi na sisi tukawa wasafi, katika mji safi wenye  kupendeza.

Friday, 19 September 2014



    E- MAIL KUTOKA KWA KOMREDI PEE CHOU

Wakati tukiwa katika ziara yetu kuzunguka Kivulini kwetu tumepokea e mail kutoka kwa rafiki yetu komredi Pee Chou ambayo kutokana na uzito wa ujumbe uliokuwemo tumeonelea tuuweke wazi ili angalau na wapenzi wa Kivulini kwetu muweze na nyinyi kupata vionjo vyake.

Ujumbe huu ulikuwa ni wa  kutusalimu na juu ya salamu hizo ulikuwa ukieleza mambo yafuatayo:

1.           Ndugu Pee Chou alikuwa akitupa pole kwa misukosuko ambayo tunakabiliana nayo kwa sasa ya  kiuchumi, kijamii na hasahasa kisiasa.


2.          Ndugu yetu alikuwa akitutahadharisha kwa kutueleza kuwa tukiendelea kucheka na manyani basi  tujiandae kuvuna mabua. Alidai huko kwao hawaoni aibu kumzamisha baharia mmoja au nahodha mkorofi ili mradi kuhakikisha kuwa meli imefika nchi kavu salama iliwa na abiria   wengi.


3.          Ndugu yetu alituonya sana kuhusu suala la kuwa wema kupita uwezo. Alitushangaa 
             sana tunapokuwa waungwana hata kwa watu wasiokuwa na fadhira wala staha.
            Alisema huko kwao wakitaka kumwua nyani hawamwangalii
             usoni.


4.          Pee Chou alituonya juu ya imani yetu kuwa sisi tumebarikiwa na ni nchi teule ambayo haitakuja kuharibika siku zijazo. Alituasa sana sana tusijidanganye. Amani siku zote hulindwa kwa gharama zozote kwa sababu siku ikipotea ni kama kudondosha sindano ndogo usiku kwenye msitu wa nyasi.


5.         Ndugu yetu alituonya tusiwaendekeze watu ambao kwanza hawana hata faida kwa nchi. Aliomba tumjali sana mzalendo na mpenda nchi na yeyote mpenda fujo na vurugu azomewe na kudhibitiwa mapema kabla hajaleta madhara katika nchi kwa sababu ujinga wa mtu mmoja unaweza kuliangamiza taifa zima.


6.         Pee Chou alisema kuwa tusisahau kuwa kitulacho ki nguoni mwetu.

 Hayo ndiyo yaliyokuwemo katika e mail hiyo. Sisi wa Kivulini kwetu hatuna maoni yoyote juu ya e  -  mail hiyo zaidi ya kumshukuru ndugu yetu Pee Chou kwa kututumia maoni haya kwa 
 wakati muafaka.

URASIMU BENKI



         URASIMU WA BENKI

Katika Ziara ya jopo la Kivulini kwetu, kitu cha kwanza kupambana nacho kilikuwa ni kero ya urasimu wa Banki. Ilikuwa ni kero ya kwanza kwa sababu kabla ya yote kikundi hiki kililazimika  kupata fedha kwa ajili ya safari ambayo walikuwa wamekusudia kuifanya.

Jamaa hawa walipokwenda Benki walishangaa sana walipopambana na mambo ambayo hawakutarajia kuyakuta yakitendeka katika karne hii ya utandawazi iliyojaa wasomi na watu waliokaramka.

Kipindi walichokwenda benki kilikuwa ni kipindi cha mwisho wa mwezi na benki waliyokwenda ni miongoni mwa benki maarufu ambazo wafanyakazi hupitishia mishahara yao huko.




Katika tawi walilokwenda kulikuwa na takribani madirisha nane ya kutolea huduma za kuweka na kutoa fedha. Lakini kitu cha kushangaza ni kuwa madirisha yaliyokuwa yakitoa huduma yalikuwa ni mawili tu na mengine sita yalikuwa hayana wahudumu. Matokeo ya hali ile ni kuwa kulikuwa na msururu mrefu ambao ulikuwa umezunguka kujaa ndani ya benki na hadi kutoka nje. Huko nje ulipandana na msururu uliokuwa ukisubiri kutoa pesa kwa kutumia mashine za ATM.



Utaratibu huu mbovu wa kuweka wahudumu wachache kipindi ambacho kuna wateja wengi kilikuwa  ni usumbufu  na udharirishaji wa hali ya juu kwa wateja. Ili kupata fedha mtu ilimlazimu kusota kwa takribani masaa matatu kwani hata hao watoa  huduma wawili walikuwa wakifanya kazi hiyo kwa taratibu kana kwamba hawaoni umati uliokuwepo.

Katika hali hii wapo walioamua kwenda zao na fedha zao na wengine kuondoka na shida zao kwani kwa hakika utaratibu huu ulikuwa unachosha na kukera.

Kitu cha kujiuliza ni kuwa hivi ni kweli benki hizi zinakotupeleka ndiko tunakotaka ? Katika kipindi hiki cha ushindani wa huduma bado wao hawaoni umuhimu wa kubadilika ? Ama wanatulazimisha tulipane hata mishahara kwa kupitia M-Pesa, Tigo Pesa n.k.; kwa sababu haina maana wala haiingii akilini kwa karne hii kutumia hata nusu saa tu kupata huduma ya benki katika msongamano huu wa teknolojia na weledi. Na kwanini mtu fedha yake imtese kiasi hicho. Wakati mwingine wengine wana dharura, wagonjwa ama wanazo ratiba zao.


Tunaomba sana na tunawasihi ndugu zetu wa Benki kama wanatusikia waachane na urasimu huu ambao umepitwa na wakati kabisa. Kama wanadhani hawawahitaji wateja basi watoe matangazo wasitumie usemi wa AKUFUKUZAYE HAKWAMBII TOKA.




       TAARIFA YA KUREJEA KUTOKA SAFARI




Baada ya kupotea kwa karibu viki tatu, kikosi kazi cha Kivulini kwetu kimerejea tena ulingoni kuendelea na kuwapatia taarifa mbalimbali za siku hadi siku kwa malengo yale yale ya kuwaelimisha kuwahabarisha na kuwaburudisha ili wanachama wetu na wapenzi muweze kupata kile ambacho roho zenu zinataka.

Kwa kipindi chote hicho ambacho hatukuwa hewani, tulikuwa katika ziara ndefu ya kutembelea maeneo mbalimbali ya Kivulini kwetu ili kujionea jinsi maisha ya jamii yetu yanavyokwenda. Katika ziara hii tumeona mengi ambayo kwa faida ya jamii yetu tutakuwa tukiwapasha moja baada ya jingine. Tunaomba ushirikiano wenu.