SUALA LA UCHAFU
Kivulini kwetu safari hii tunataka kuongelea suala la uchafu
katika mji wetu. Suala hili limekuwa kama tabia na inaelekea tabia hii
inaimarika sana na kuwa utamaduni wa jamii yetu.
Kama tujuavyo uchafu ni takataka; lakini pia uchafu ni hali ya
kutokuwa msafi. Uchafu pia inaweza kuwa tabia ya mtu au watu kutokuwa wasafi.
Wakati tukitathmini uchafu kuna namna nyingi ya mtu au watu
kutokuwa wasafi.
Namna ya kwanza ambayo ni rahisi kuelezeka ni tabia ya watu
kutoona kinyaa kukaa katika mazingira yenye takataka kama vile masalia ya
matunda, matambara, makaratasi na kadharika. Lakini pia kukaa mahali penye
uvundo ama panapotiririka maji machafu, kwenye mifereji michafu na kadharika.
Uchafu mwingine ni tabia ya kutotunza mazingira kwa kutupa
taka ovyo, kula ovyo, kuvaa ovyo na kadharika.
Uchafu mwingine ni kutokuwa na mpangilio mzuri wa vitu hata
kama vitu hivyo ni visafi. Mfano katika mji ni kuegesha magari ovyo, kupanga
bidhaa ovyo hadi barabarani, ujenzi holela, migongamano isiyo ya lazima,
kufanya shughuli zozote mahali pasipostahili kama kupika sehemu za wazi, kulala
kwenye mavaranda, kuosha magari barabarani, gereji kwenye makazi ya watu, vituo
vya mafuta kwenye makazi ya watu, viwanda vya jua kali mahali pasipostahili na
mengine mengi ya aina hiyo
.
Baada ya kufuatilia kwa karibu tumegundua kuwa chanzo cha
hali hii ni mamlaka husika za mji kutowajibika katika kusimamia sheria na
taratibu za mji. Aidha si kutosimamia tu bali kutokuwa na mipango au utaratibu
endelevu katika kuuweka mji namna unavyopasa kuwa.
Mamlaka zimeshindwa kutoka maelekezo fasaha na kwa wakati
juu ya kipi kifanyike, wapi kifanyike, nani afanye na afanye wakati gani. Na
juu ya hayo kueleza wazi kuwa atakayekiuka maelekezo hayoatafanywa nini na
kweli inapotokea mtu kakiuka basi hatua zichukuliwe.
Kinachojitokeza ni kusimamia machache baadhi na kusimamia
kwake ni kinyume na inavyotakiwa; kwamba upo upendeleo kwa baadhi ya watu, kwa
baadhi ya maeneo na baadhi tu na masuala yote yanayotakiwa kusimamiwa. Matokeo
ya kufanya hivi ni jamii nzima kuachwa njiapanda watu wasijue ni kipi sahihi
kufanyika na nani anapaswa kufanya kwani katika eneo moja, watu wa aina moja,
katika muda unaofanana; wapo wanaoruhusiwa kufanya na wapo wanaozuiwa kufanya
kitu kilekile, mahali palepale na katika muda uleule.
Chanzo kingine cha uchafu ni tabia ya mtu mmoja mmoja ya
uchafu. Hii inatokana aidha na malezi, ukosefu wa elimu, umaskini na mlengo wa
kushoto wa mawazo.
Kitendo cha mtu kula matunda na kutupa maganda barabarani,
kitendo cha mtu kunywa maji au soda na kutupa chupa katika mfereji, tabia ya
mtu kuuza bidhaa zake dukani na makasha, maboksi, na vifungio vingine ovyo
mbele ya duka lake, vitendo vya watu kujisaidia haja kuwa na ndogo katika
mifereji ya majitaka wakati mwingine mchana kweupe, vitendo vya kupanga bidhaa
za chakula juu ya maji yanayotiririka na kuwauzia watu na hata wao pia kununua;
lakini mbaya zaidi kitendo cha kuona haya yote yanafanyika na kuacha kuyakemea;
yate haya yanajumuika katika tabia ya uchafu. Watu wamekuwa hawaoni vibaya juu
ya masuala haya na imekuwa ni kawaida.
Hujitokeza kuacha kwa muda pindi
wanapotangaziwa na mamlaka waache kutokana pengine na milipuko ya magonjwa ama
kuwe na ugeni unakuja Kivulini kwetu. Katika harakati hizo za kuzuia uchafu
watu hulalamika sana kuwa wanaonewa na kunyanyaswa katika nchi yao kwa kuambiwa
waachane na uchafu. Baada ya milipuko na ugeni kuondoka hali ya uchafu hurejea
mahali pake. Kwa hakika inasikitisha sana.
Binafsi nilidhani ipo haja kwanza ya jamii ambamo na wenye
mamlaka wanatoka humo ibadilike na kuchukia mazingira machafu. Tuwe jamii yenye
kuona kinyaa kukaa kwenye majalala,
kutupa taka ovyo, kujisaidia ovyoovyo, kununua vitu vichafu, kuvaa mavazi
machafu, sisi wenyewe kutokuwa wachafu; kwa sababu nakumbuka kuna siku alipanda
mtu mmoja kwenye daladala(simtaji jina, siitaji jinsia yake, dini yake wala
kabila japo niliulizia na vyote nikaambiwa) kila abiria ilibidi afunge pua;
lakini hiyo haikutosha wakaomba mtu huyo ashushwe vinginevyo wao washuke;
ikabidi ashushwe kituo kinachofuata; kwani kwa jinsi alivyokuwa ananuka ni
afadhari ya kinyesi; unaweza kupata hiyo picha kuwa mtu huyu anatoka wapi na
amewakera watu kiasi gani katika maeneo yote aliyopita. Mtu kama huyu kuna
uchafu gani utakaomtisha akaogopa ?
Lakini juu ya jamii kujirekebisha, mamlaka nazo ziweke
utaratibu mzuri wa kufuatwa. Kuwe na sheria za kufuatwa ili kuweka mji katika
usafi. Taratibu zizuie baadhi ya mambo yanayosababisha uchafu kufanyika na
taratibu hizo zisimamiwe bila ya ubaguzi wala upendeleo na usimamizi huo uwe
endelevu na sio zima moto.
Ninasali ije itokee kipindi na sisi tukawa wasafi, katika
mji safi wenye kupendeza.
No comments:
Post a Comment