Friday, 19 September 2014

URASIMU BENKI



         URASIMU WA BENKI

Katika Ziara ya jopo la Kivulini kwetu, kitu cha kwanza kupambana nacho kilikuwa ni kero ya urasimu wa Banki. Ilikuwa ni kero ya kwanza kwa sababu kabla ya yote kikundi hiki kililazimika  kupata fedha kwa ajili ya safari ambayo walikuwa wamekusudia kuifanya.

Jamaa hawa walipokwenda Benki walishangaa sana walipopambana na mambo ambayo hawakutarajia kuyakuta yakitendeka katika karne hii ya utandawazi iliyojaa wasomi na watu waliokaramka.

Kipindi walichokwenda benki kilikuwa ni kipindi cha mwisho wa mwezi na benki waliyokwenda ni miongoni mwa benki maarufu ambazo wafanyakazi hupitishia mishahara yao huko.




Katika tawi walilokwenda kulikuwa na takribani madirisha nane ya kutolea huduma za kuweka na kutoa fedha. Lakini kitu cha kushangaza ni kuwa madirisha yaliyokuwa yakitoa huduma yalikuwa ni mawili tu na mengine sita yalikuwa hayana wahudumu. Matokeo ya hali ile ni kuwa kulikuwa na msururu mrefu ambao ulikuwa umezunguka kujaa ndani ya benki na hadi kutoka nje. Huko nje ulipandana na msururu uliokuwa ukisubiri kutoa pesa kwa kutumia mashine za ATM.



Utaratibu huu mbovu wa kuweka wahudumu wachache kipindi ambacho kuna wateja wengi kilikuwa  ni usumbufu  na udharirishaji wa hali ya juu kwa wateja. Ili kupata fedha mtu ilimlazimu kusota kwa takribani masaa matatu kwani hata hao watoa  huduma wawili walikuwa wakifanya kazi hiyo kwa taratibu kana kwamba hawaoni umati uliokuwepo.

Katika hali hii wapo walioamua kwenda zao na fedha zao na wengine kuondoka na shida zao kwani kwa hakika utaratibu huu ulikuwa unachosha na kukera.

Kitu cha kujiuliza ni kuwa hivi ni kweli benki hizi zinakotupeleka ndiko tunakotaka ? Katika kipindi hiki cha ushindani wa huduma bado wao hawaoni umuhimu wa kubadilika ? Ama wanatulazimisha tulipane hata mishahara kwa kupitia M-Pesa, Tigo Pesa n.k.; kwa sababu haina maana wala haiingii akilini kwa karne hii kutumia hata nusu saa tu kupata huduma ya benki katika msongamano huu wa teknolojia na weledi. Na kwanini mtu fedha yake imtese kiasi hicho. Wakati mwingine wengine wana dharura, wagonjwa ama wanazo ratiba zao.


Tunaomba sana na tunawasihi ndugu zetu wa Benki kama wanatusikia waachane na urasimu huu ambao umepitwa na wakati kabisa. Kama wanadhani hawawahitaji wateja basi watoe matangazo wasitumie usemi wa AKUFUKUZAYE HAKWAMBII TOKA.

No comments:

Post a Comment