FACEBOOK
Leo Kivulini kwetu tulikuwa na mjadala kuhusu mitandao
hususani mtandao wa Facebook. Tulikuwa tukijaribu kufanya tathmini ili kuona ni kwa kiasi gani mitandao hii
inatusaidia hasa sisi wa nchi zinazoendelea.
Kwanza tulipitia akaunti nyingi na kukuta idadi kubwa ya
akaunti hizo zina walakini. Kulikuwa na akaunti nyingi sana ambazo hazikuwa na
majina ya kweli. Kulikuwa na akaunti nyingi ambazo hazikuwa na picha za kweli
za wahusika. Kulikuwa na akaunti nyingi ambazo badala ya picha za watu kulikuwa
na picha za maboksi, miti, bendera, wanyama, maua n.k. Kulikuwa na baadhi ya
akaunti zilikuwa na jina moja lakini picha ni ya kikundi na hivyo kuwa vigumu
kumjua mwenye jina husika ni nani.
Lakini zipo akaunti ambazo zilikuwa ni za halali kwa kila hali.
Utafiti huo kwanza ulituthihirishia kuwa pindi akaunti hizo
zilikuwa ni za mizengwe, hata mawazo na uchangiaji wake katika facebook wa hao
waongo pia ulikuwa ni wa bandia. Mengi
yaliyokuwa yakielezwa hayakuwa mawazo halisi au mitizamo thabiti. Uchangiaji
mwingi ni wa kufuata mkumbo, kijipendekeza, ushabiki njaa, na kejeli.
Kivulini kwetu hatukuwa na nia ya kuingilia uhuru wa mtu
wala kukinzana na maboresho ya utandawazi bali tulikuwa tukitaka
kujithibitishia kuwa fulsa hii ya mitandao ya jamii imetusaidiaje kwa mtu mmoja
mmoja. Ili kupata picha ya nini kipo katika facebook na faida zake nitatoa
mifano midogo mitatu.
1. Kuna siku mtu aliweka picha ya jeneza kwenye ukurasa
wake. Watu zaidi ya mia tano wali like. Sijaelewa wali like kwa sababu ya
urafiki na aliyeliweka ama wali like kwa kulipenda sana jeneza ama vipi. Lakini
iwe iwavyo bila ya hata mmoja wapo kutoa maoni yoyote inatia shaka.
2. Inatokea dada anaweka picha yake. Baada ya sekunde
kunamiminika like, sifa, na kashfa kibao mpaka wakati mwingine anaamua
kuiondoa.
3. Anatokea mtu anaandika neno moja tu NAOMBA; zaidi ya watu
elfu watachangia kwa sentesi mojamoja au neno mojamoja. Baada ya mjadala kwisha
ndiyo hadithi imekwisha.
Sasa unaweza kukuta mtu kashinda ana facebook lakini
hajapata rafiki, hajapata mchumba, hajafanya biashara, hajaongeza japo elimu
kidogo ya chochote, hajatoa mawazo wala kuelimisha chochote lakini bando
limekwenda, muda umekwenda, macho yameingia giza na vidole vimewasha. Sasa huu
mtandao unakuwa umekuweka wapi katika ulimwengu wa sasa.
Hii ni mada inayotugusa wengi sana, na lazima tukasirike
kidogo; lakini ukweli unabaki palepale kuwa hatuitumii vizuri hii mitandao.
Wenzetu wanauza, wananunua, wanaelimika, wanaelimisha, wanatafuta na wanapata
watakavyo kupitia mitandao. Ndugu zangu tusikubali siku ipite hujajifunza au
kupata chochote cha nyongeza kutoka katika mtandao.
No comments:
Post a Comment