Friday, 19 September 2014



    E- MAIL KUTOKA KWA KOMREDI PEE CHOU

Wakati tukiwa katika ziara yetu kuzunguka Kivulini kwetu tumepokea e mail kutoka kwa rafiki yetu komredi Pee Chou ambayo kutokana na uzito wa ujumbe uliokuwemo tumeonelea tuuweke wazi ili angalau na wapenzi wa Kivulini kwetu muweze na nyinyi kupata vionjo vyake.

Ujumbe huu ulikuwa ni wa  kutusalimu na juu ya salamu hizo ulikuwa ukieleza mambo yafuatayo:

1.           Ndugu Pee Chou alikuwa akitupa pole kwa misukosuko ambayo tunakabiliana nayo kwa sasa ya  kiuchumi, kijamii na hasahasa kisiasa.


2.          Ndugu yetu alikuwa akitutahadharisha kwa kutueleza kuwa tukiendelea kucheka na manyani basi  tujiandae kuvuna mabua. Alidai huko kwao hawaoni aibu kumzamisha baharia mmoja au nahodha mkorofi ili mradi kuhakikisha kuwa meli imefika nchi kavu salama iliwa na abiria   wengi.


3.          Ndugu yetu alituonya sana kuhusu suala la kuwa wema kupita uwezo. Alitushangaa 
             sana tunapokuwa waungwana hata kwa watu wasiokuwa na fadhira wala staha.
            Alisema huko kwao wakitaka kumwua nyani hawamwangalii
             usoni.


4.          Pee Chou alituonya juu ya imani yetu kuwa sisi tumebarikiwa na ni nchi teule ambayo haitakuja kuharibika siku zijazo. Alituasa sana sana tusijidanganye. Amani siku zote hulindwa kwa gharama zozote kwa sababu siku ikipotea ni kama kudondosha sindano ndogo usiku kwenye msitu wa nyasi.


5.         Ndugu yetu alituonya tusiwaendekeze watu ambao kwanza hawana hata faida kwa nchi. Aliomba tumjali sana mzalendo na mpenda nchi na yeyote mpenda fujo na vurugu azomewe na kudhibitiwa mapema kabla hajaleta madhara katika nchi kwa sababu ujinga wa mtu mmoja unaweza kuliangamiza taifa zima.


6.         Pee Chou alisema kuwa tusisahau kuwa kitulacho ki nguoni mwetu.

 Hayo ndiyo yaliyokuwemo katika e mail hiyo. Sisi wa Kivulini kwetu hatuna maoni yoyote juu ya e  -  mail hiyo zaidi ya kumshukuru ndugu yetu Pee Chou kwa kututumia maoni haya kwa 
 wakati muafaka.

URASIMU BENKI



         URASIMU WA BENKI

Katika Ziara ya jopo la Kivulini kwetu, kitu cha kwanza kupambana nacho kilikuwa ni kero ya urasimu wa Banki. Ilikuwa ni kero ya kwanza kwa sababu kabla ya yote kikundi hiki kililazimika  kupata fedha kwa ajili ya safari ambayo walikuwa wamekusudia kuifanya.

Jamaa hawa walipokwenda Benki walishangaa sana walipopambana na mambo ambayo hawakutarajia kuyakuta yakitendeka katika karne hii ya utandawazi iliyojaa wasomi na watu waliokaramka.

Kipindi walichokwenda benki kilikuwa ni kipindi cha mwisho wa mwezi na benki waliyokwenda ni miongoni mwa benki maarufu ambazo wafanyakazi hupitishia mishahara yao huko.




Katika tawi walilokwenda kulikuwa na takribani madirisha nane ya kutolea huduma za kuweka na kutoa fedha. Lakini kitu cha kushangaza ni kuwa madirisha yaliyokuwa yakitoa huduma yalikuwa ni mawili tu na mengine sita yalikuwa hayana wahudumu. Matokeo ya hali ile ni kuwa kulikuwa na msururu mrefu ambao ulikuwa umezunguka kujaa ndani ya benki na hadi kutoka nje. Huko nje ulipandana na msururu uliokuwa ukisubiri kutoa pesa kwa kutumia mashine za ATM.



Utaratibu huu mbovu wa kuweka wahudumu wachache kipindi ambacho kuna wateja wengi kilikuwa  ni usumbufu  na udharirishaji wa hali ya juu kwa wateja. Ili kupata fedha mtu ilimlazimu kusota kwa takribani masaa matatu kwani hata hao watoa  huduma wawili walikuwa wakifanya kazi hiyo kwa taratibu kana kwamba hawaoni umati uliokuwepo.

Katika hali hii wapo walioamua kwenda zao na fedha zao na wengine kuondoka na shida zao kwani kwa hakika utaratibu huu ulikuwa unachosha na kukera.

Kitu cha kujiuliza ni kuwa hivi ni kweli benki hizi zinakotupeleka ndiko tunakotaka ? Katika kipindi hiki cha ushindani wa huduma bado wao hawaoni umuhimu wa kubadilika ? Ama wanatulazimisha tulipane hata mishahara kwa kupitia M-Pesa, Tigo Pesa n.k.; kwa sababu haina maana wala haiingii akilini kwa karne hii kutumia hata nusu saa tu kupata huduma ya benki katika msongamano huu wa teknolojia na weledi. Na kwanini mtu fedha yake imtese kiasi hicho. Wakati mwingine wengine wana dharura, wagonjwa ama wanazo ratiba zao.


Tunaomba sana na tunawasihi ndugu zetu wa Benki kama wanatusikia waachane na urasimu huu ambao umepitwa na wakati kabisa. Kama wanadhani hawawahitaji wateja basi watoe matangazo wasitumie usemi wa AKUFUKUZAYE HAKWAMBII TOKA.




       TAARIFA YA KUREJEA KUTOKA SAFARI




Baada ya kupotea kwa karibu viki tatu, kikosi kazi cha Kivulini kwetu kimerejea tena ulingoni kuendelea na kuwapatia taarifa mbalimbali za siku hadi siku kwa malengo yale yale ya kuwaelimisha kuwahabarisha na kuwaburudisha ili wanachama wetu na wapenzi muweze kupata kile ambacho roho zenu zinataka.

Kwa kipindi chote hicho ambacho hatukuwa hewani, tulikuwa katika ziara ndefu ya kutembelea maeneo mbalimbali ya Kivulini kwetu ili kujionea jinsi maisha ya jamii yetu yanavyokwenda. Katika ziara hii tumeona mengi ambayo kwa faida ya jamii yetu tutakuwa tukiwapasha moja baada ya jingine. Tunaomba ushirikiano wenu.

Wednesday, 3 September 2014



           FACEBOOK

Leo Kivulini kwetu tulikuwa na mjadala kuhusu mitandao hususani mtandao wa Facebook. Tulikuwa tukijaribu kufanya tathmini  ili kuona ni kwa kiasi gani mitandao hii inatusaidia hasa sisi wa nchi zinazoendelea.



Kwanza tulipitia akaunti nyingi na kukuta idadi kubwa ya akaunti hizo zina walakini. Kulikuwa na akaunti nyingi sana ambazo hazikuwa na majina ya kweli. Kulikuwa na akaunti nyingi ambazo hazikuwa na picha za kweli za wahusika. Kulikuwa na akaunti nyingi ambazo badala ya picha za watu kulikuwa na picha za maboksi, miti, bendera, wanyama, maua n.k. Kulikuwa na baadhi ya akaunti zilikuwa na jina moja lakini picha ni ya kikundi na hivyo kuwa vigumu kumjua mwenye jina  husika ni nani. Lakini zipo akaunti ambazo zilikuwa ni za halali kwa kila hali.



Utafiti huo kwanza ulituthihirishia kuwa pindi akaunti hizo zilikuwa ni za mizengwe, hata mawazo na uchangiaji wake katika facebook wa hao waongo pia ulikuwa ni wa bandia.  Mengi yaliyokuwa yakielezwa hayakuwa mawazo halisi au mitizamo thabiti. Uchangiaji mwingi ni wa kufuata mkumbo, kijipendekeza, ushabiki njaa, na kejeli.



Kivulini kwetu hatukuwa na nia ya kuingilia uhuru wa mtu wala kukinzana na maboresho ya utandawazi bali tulikuwa tukitaka kujithibitishia kuwa fulsa hii ya mitandao ya jamii imetusaidiaje kwa mtu mmoja mmoja. Ili kupata picha ya nini kipo katika facebook na faida zake nitatoa mifano midogo mitatu.

1. Kuna siku mtu aliweka picha ya jeneza kwenye ukurasa wake. Watu zaidi ya mia tano wali like. Sijaelewa wali like kwa sababu ya urafiki na aliyeliweka ama wali like kwa kulipenda sana jeneza ama vipi. Lakini iwe iwavyo bila ya hata mmoja wapo kutoa maoni yoyote inatia shaka.

2. Inatokea dada anaweka picha yake. Baada ya sekunde kunamiminika like, sifa, na kashfa kibao mpaka wakati mwingine anaamua kuiondoa.

3. Anatokea mtu anaandika neno moja tu NAOMBA; zaidi ya watu elfu watachangia kwa sentesi mojamoja au neno mojamoja. Baada ya mjadala kwisha ndiyo hadithi imekwisha.

Sasa unaweza kukuta mtu kashinda ana facebook lakini hajapata rafiki, hajapata mchumba, hajafanya biashara, hajaongeza japo elimu kidogo ya chochote, hajatoa mawazo wala kuelimisha chochote lakini bando limekwenda, muda umekwenda, macho yameingia giza na vidole vimewasha. Sasa huu mtandao unakuwa umekuweka wapi katika ulimwengu wa sasa.



Hii ni mada inayotugusa wengi sana, na lazima tukasirike kidogo; lakini ukweli unabaki palepale kuwa hatuitumii vizuri hii mitandao. Wenzetu wanauza, wananunua, wanaelimika, wanaelimisha, wanatafuta na wanapata watakavyo kupitia mitandao. Ndugu zangu tusikubali siku ipite hujajifunza au kupata chochote cha nyongeza kutoka katika mtandao.