Monday, 8 February 2016

WANAMUZIKI NA MA-DJ EBU NENDENI NA MATUKIO

Kwa hakika Kivulini kwetu tuna mengi sana ya kuzungumza. Kama mjuavyo sisi ni wanajamii na kila wakati hujaribu kushauri kila panapojitokea mahitaji ya ushauri; yote ikiwa ni kwa lengo la kuboresha mambo.

Ni ukweli usiopingika kuwa kila panapo shughuli muziki huwa ni moja ya vitu muhimu. Waweza kuwa ni muziki toka kwa wanamuziki moja kwa moja au muziki kupitia vyombo mahsusi.

Tuliloliona katika hayo ni kutokuwepo uangalifu wa wafanya muziki katika kuoanisha shughuli husika na muziki unaopigwa na pia kupimia unenguaji na ukatikaji kulingana na hadhara inayohusika.

Unaweza kwenda bar na kukuta nyimbo za kanisani zinapigwa. Unaweza kwenda kwenye kampeni za uchaguzi ukakuta bendi inaimba nyimbo za mapenzi, vijembe ya mitaani au maombolezo mengine ya kijamii. Unaweza kwenda harusini ukakuta wanapiga nyimbo za siasa za chama fulani. Unaweza pia kwenda kwenye mahafali fulani ukakuta hakujapigwa hata wimbo mmoja unagusia elimu. Hii ndiyo hali iliyopo kwa wanamuziki wetu na waandaaji wa shughuli hizo.

Kivulini kwetu tunajiuliza hivi mwanamuziki anayemwimba mpenzi wake katika sherehe au maadhimisho ya kitaifa wakati alipewa taarifa ya miezi kadhaa juu ya shughuli hiyo haoni kuwa ana mapungufu ? Kwanini hakuuliza afahamishwe maudhui ya sherehe ili aweze kuandaa nyimbo au wimbo wa shughuli hiyo.

Na huyu DJ anayetuwekea muziki wa kumsifu kiongozi wa chama cha siasa kwenye harusi yetu ni nani kamwambia kuwa wote walioalikwa ni wa chama hicho na hata kama yanahusiana vipi mambo hayo.

Hivi neno la bwana kuibwa mbele ya walevi wanaofakamia viloba huku wakijifanya kucheza kwa hisia sio matumizi mabaya ya nyimbo hizo. Hata kama wanadai kuwa hao ndio wanaohitajika kukombolewa lakini kweli ?

Jambo hili limekomaa na linakera kiasi chake; sisi tunashauri wanamuziki wakomae sasa na kujitahidi kuoanisha miziki yao na matukio kwani kuna kipindi hasa cha kampeni ilikuwa inafikia mpaka unaombea umeme ukatike au mitambo ikorofishe aache kuimba vituko. Mwanamuziki anajisahau kwa kuimba mambo yake mbele za viongozi na watu wenye heshima zao na hata uchezaji ulikuwa hauendani na hadhara zile; kisa kaalikwa aje kwenye kampeni.

Kivulini kwetu tunawapenmda sana wana muziki na ndiyo maana tunatumia muda wetu kuwashauri kwa sababu tunaamini kuwa aibu yenu ndiyo aibu yetu. 

Tunawashauri mnapokuwa kwenye viwanja vyenu fanyeni mnavyojua lakini muwapo nje kwenye hadhara iliyochanganyika imbeni ya hadhara, vaeni vizuri na chezeni kiungwana mkizingatia kuwa nyie ndiyo kioo cha jamii.

No comments:

Post a Comment