Monday, 8 February 2016

SINEMA ZA KISWAHILI YENYE MAJINA YA KIZUNGU


Kwa mara nyingine tena Kivulini kwetu tumeamua kueleza hisia zetu juu ya utaratibu huu ambao tunadhani una kasoro kubwa ndani yake.

Kwa kipindi kirefu sasa tumeshuhudia wasanii wetu wakifyatua sinema nyingi zenye majina ya kizungu/kiingereza ilhali lugha inayotumika katika kuigiza ni kiswahili.

Tuliwahi siku za nyuma kuhoji juu ya suala hili na majibu yaliyotoka yalikuwa ni sababu za kibiashara; kwamba sinema ikiandikwa jina kwa kiswahili inakuwa haivutii sana kama ambavyo ingeliandikwa kwa lugha aya kigeni. 

Kivulini kwetu hatujatosheka na sababu hiyo kwa sababu wateja wengi wa sinema hizo ni sisi na kama wanaona zinanunuliwa sana wajue si kwa sababu za majina ya kiingereza bali ubora wa picha na sauti na pia uzoefu ambao umekuwepo kwa waigizaji wetu. Najisikia aibu kuona tunajikana wenyewe kwa kuamini kuwa kwa kuchanganya lugha tunakitendea haki kiswahili ama kiingereza.

Pangine tungelichukua mfano wa Nigeria ambapo kuna kipindi sinema zao zilikuwa na soko sana hapa kwetu; sikumbuki kuona wakibadili majina ya sinema zao kuwa ya kiswahili; lakini sisi wapenzi bila kujali hilo tulikuwa walevi wa sinema zao.

Ushauri wetu kwa wasanii wetu kama kweli wanalitaka soko la Ulaya la sinema basi waigize sinema zao kwa lugha ya kizungu na hivyo kuleta mantiki ya kutumia majina ya kizungu na si kuchomekea maneno ambayo nayo huwa ya kama kubahatisha fulani, kuchomekea uzungu ulio nje ya maadili na kuonyesha maisha fulani ambayo hayapo katika jamii yetu.

Yapo mengi ya kusahihisha lakini hili tulidhani lina umuhimu zaidi kushinda hayo mengine ambayo si ya kutisha sana.

Hata hivyo tutakuwa wachoyo wa fadhila kutowapongeza waigizaji wetu kwa juhudi wanazofanya angalau sasa hivi kazi zao zina ubora. Ila wasikimbilie sana kutoa sinema zenye maandalizi hafifu ili kubakiza imani kwa wateja kuwa kazi zao zi la kulipua. Wasirekodi sinema kwa mapenzi yao bali warekodi kwa mapenzi yetu kwani mwisho wa siku sisi ndio tutakaozinunua na kuzitazama sinema hizo. Wasikusanye mashangazi, majirani na marafiki ili nao wauze sura; wakumbuke hiyo ni kazi na inahitaji kuheshimiwa.

No comments:

Post a Comment