Monday, 8 February 2016

WANAMUZIKI NA MA-DJ EBU NENDENI NA MATUKIO

Kwa hakika Kivulini kwetu tuna mengi sana ya kuzungumza. Kama mjuavyo sisi ni wanajamii na kila wakati hujaribu kushauri kila panapojitokea mahitaji ya ushauri; yote ikiwa ni kwa lengo la kuboresha mambo.

Ni ukweli usiopingika kuwa kila panapo shughuli muziki huwa ni moja ya vitu muhimu. Waweza kuwa ni muziki toka kwa wanamuziki moja kwa moja au muziki kupitia vyombo mahsusi.

Tuliloliona katika hayo ni kutokuwepo uangalifu wa wafanya muziki katika kuoanisha shughuli husika na muziki unaopigwa na pia kupimia unenguaji na ukatikaji kulingana na hadhara inayohusika.

Unaweza kwenda bar na kukuta nyimbo za kanisani zinapigwa. Unaweza kwenda kwenye kampeni za uchaguzi ukakuta bendi inaimba nyimbo za mapenzi, vijembe ya mitaani au maombolezo mengine ya kijamii. Unaweza kwenda harusini ukakuta wanapiga nyimbo za siasa za chama fulani. Unaweza pia kwenda kwenye mahafali fulani ukakuta hakujapigwa hata wimbo mmoja unagusia elimu. Hii ndiyo hali iliyopo kwa wanamuziki wetu na waandaaji wa shughuli hizo.

Kivulini kwetu tunajiuliza hivi mwanamuziki anayemwimba mpenzi wake katika sherehe au maadhimisho ya kitaifa wakati alipewa taarifa ya miezi kadhaa juu ya shughuli hiyo haoni kuwa ana mapungufu ? Kwanini hakuuliza afahamishwe maudhui ya sherehe ili aweze kuandaa nyimbo au wimbo wa shughuli hiyo.

Na huyu DJ anayetuwekea muziki wa kumsifu kiongozi wa chama cha siasa kwenye harusi yetu ni nani kamwambia kuwa wote walioalikwa ni wa chama hicho na hata kama yanahusiana vipi mambo hayo.

Hivi neno la bwana kuibwa mbele ya walevi wanaofakamia viloba huku wakijifanya kucheza kwa hisia sio matumizi mabaya ya nyimbo hizo. Hata kama wanadai kuwa hao ndio wanaohitajika kukombolewa lakini kweli ?

Jambo hili limekomaa na linakera kiasi chake; sisi tunashauri wanamuziki wakomae sasa na kujitahidi kuoanisha miziki yao na matukio kwani kuna kipindi hasa cha kampeni ilikuwa inafikia mpaka unaombea umeme ukatike au mitambo ikorofishe aache kuimba vituko. Mwanamuziki anajisahau kwa kuimba mambo yake mbele za viongozi na watu wenye heshima zao na hata uchezaji ulikuwa hauendani na hadhara zile; kisa kaalikwa aje kwenye kampeni.

Kivulini kwetu tunawapenmda sana wana muziki na ndiyo maana tunatumia muda wetu kuwashauri kwa sababu tunaamini kuwa aibu yenu ndiyo aibu yetu. 

Tunawashauri mnapokuwa kwenye viwanja vyenu fanyeni mnavyojua lakini muwapo nje kwenye hadhara iliyochanganyika imbeni ya hadhara, vaeni vizuri na chezeni kiungwana mkizingatia kuwa nyie ndiyo kioo cha jamii.
SINEMA ZA KISWAHILI YENYE MAJINA YA KIZUNGU


Kwa mara nyingine tena Kivulini kwetu tumeamua kueleza hisia zetu juu ya utaratibu huu ambao tunadhani una kasoro kubwa ndani yake.

Kwa kipindi kirefu sasa tumeshuhudia wasanii wetu wakifyatua sinema nyingi zenye majina ya kizungu/kiingereza ilhali lugha inayotumika katika kuigiza ni kiswahili.

Tuliwahi siku za nyuma kuhoji juu ya suala hili na majibu yaliyotoka yalikuwa ni sababu za kibiashara; kwamba sinema ikiandikwa jina kwa kiswahili inakuwa haivutii sana kama ambavyo ingeliandikwa kwa lugha aya kigeni. 

Kivulini kwetu hatujatosheka na sababu hiyo kwa sababu wateja wengi wa sinema hizo ni sisi na kama wanaona zinanunuliwa sana wajue si kwa sababu za majina ya kiingereza bali ubora wa picha na sauti na pia uzoefu ambao umekuwepo kwa waigizaji wetu. Najisikia aibu kuona tunajikana wenyewe kwa kuamini kuwa kwa kuchanganya lugha tunakitendea haki kiswahili ama kiingereza.

Pangine tungelichukua mfano wa Nigeria ambapo kuna kipindi sinema zao zilikuwa na soko sana hapa kwetu; sikumbuki kuona wakibadili majina ya sinema zao kuwa ya kiswahili; lakini sisi wapenzi bila kujali hilo tulikuwa walevi wa sinema zao.

Ushauri wetu kwa wasanii wetu kama kweli wanalitaka soko la Ulaya la sinema basi waigize sinema zao kwa lugha ya kizungu na hivyo kuleta mantiki ya kutumia majina ya kizungu na si kuchomekea maneno ambayo nayo huwa ya kama kubahatisha fulani, kuchomekea uzungu ulio nje ya maadili na kuonyesha maisha fulani ambayo hayapo katika jamii yetu.

Yapo mengi ya kusahihisha lakini hili tulidhani lina umuhimu zaidi kushinda hayo mengine ambayo si ya kutisha sana.

Hata hivyo tutakuwa wachoyo wa fadhila kutowapongeza waigizaji wetu kwa juhudi wanazofanya angalau sasa hivi kazi zao zina ubora. Ila wasikimbilie sana kutoa sinema zenye maandalizi hafifu ili kubakiza imani kwa wateja kuwa kazi zao zi la kulipua. Wasirekodi sinema kwa mapenzi yao bali warekodi kwa mapenzi yetu kwani mwisho wa siku sisi ndio tutakaozinunua na kuzitazama sinema hizo. Wasikusanye mashangazi, majirani na marafiki ili nao wauze sura; wakumbuke hiyo ni kazi na inahitaji kuheshimiwa.

Saturday, 16 January 2016


CHONDE SIASA ISITUTAWALE

Kivulini kwetu baada ya kuridhika kuwa kwa hali ilivyo tunaweza tukatupia neno japo moja tumeamua kufanya hivyo.

Tumeamua kuongea ili kuwaasa ndugu na jamaa zetu wajitahidi kutawala mambo yao badala ya mambo yao kuwatawala. Tuutawale ulevi na ulevi usitutawale. Tutawale lugha yetu na lugha isitutawale. Tutawale furaha yetu na furaha isitutawale. Tuutawale uhuru wetu na uhuru usitutawale. Yapo mengi katika maisha yetu ambayo ni busara sisi kuyatawala na kamwe tusiache yatutawale.

Moja ya mambo ambayo tulipenda kuyaongelea leo ni kushauri tuitawale siasa na tusiache siasa itutawale.

Tumeanza na siasa kwa sababu sasa hivi imekuwa kero; maisha yetu yamezingira na siasa kiasi kwamba tumekuwa walevi wa siasa. Siku hizi watu wanaamini kuwa mtu anaweza kutembea ki-UKAWA; anaweza kuongea ki- CCM; anaweza kula ki-CUF na kadharika. Tumefika mahala hatujiwezi mbele ya siasa; siasa imetutawala badala ya sisi kuitawala.

Yote tunayoyafanya sasa yalikuwa yakifanyika toka zamani; lakini sasa hivi tumenasa. Kila tendo limekuwa na tafsiri ya siasa. 

Zamani makabila yalikuwa yakitaniana; wachaga kwa wapare; wasukuma kwa wazaramo; wahehe kwa wangoni; wahaya kwa wakurya; ilikuwa ni kawaida sana. Walikuwa wenyewe wanajua mwanzo wa mipaka ya utani wao na mwisho wa mipaka hiyo na maisha yalikuwa yanakwenda murua kabisa.

Inashangaza ni shetani gani kaingia kiasi kwamba sasa hivi Mkwere akimtania Mnyamwezi anadaiwa anamdhalilisha; au Mgogo akimdhihaki Mrangi anakuwa kafanya kosa. Na bora basi hasira hizi zingekuwa za kawaida; sasa hivi zinaingizwa katika siasa na vyama.

Hapo nyuma kulikuwa na utani wa makabila, utani wa kuhusiana, na utani wa utaifa. Ilikuwa hushangai ukimkuta Mmakonde anasifu ubahili wa Mpare au mchaga anamsifia mnyamwezi kwamba anastahili kupewa mizigo mizito "mzigo mzito mpe Mnyamwezi"; ama Mchaga alipokuwa akisifiwa kwa kupenda pesa;  wao wahusika wa sifa hizo walilijua hilo na kwa kiasi walijisikia fahari na utani huo.

Sasa tunauliza huyo shetani ambaye anahusisha makabila na vyama katoka wapi. Nani anayetaka kuwaaminisha watu kuwa Wachaga wote ni UKAWA, Wapemba wote ni CUF, Waha wote ni ACT au Wafipa wote ni CCM kiasi kwamba wakitaniwa vinakuwa vyama vyao vimedhalilishwa.

Kuna watu wamekazana sana na biashara hiyo kiasi kwamba wanataka sasa siasa itutawale na itutoe katika tamaduni zetu na mahusianmo yetu ya asili na kutufanya tuanze kuogopana. Tusikubali.

Kivulini kwetu tulidhani tuanze mwaka kwa kulikemea jambo  hili kwani bila ya kufanya hivyo hawa jamaa ambao kwa kigezo cha kutetea udhalilishaji wa makabila wanapandikiza chuki na kuchonganisha makabila kwa minajili ya kukonga nyoyo zao kisiasa. Tukatae kutawaliwa na siasa.

Yapo mambo ambayo tukiyafanya yana manufaa lakini hili la upotoshaji wa mila zetu kamwe hazitatufikisha popote. Ni vizuri tukapuuza tafsiri hizi na kupambana tubaki katika mstari wetu wa mahusiano.

Wednesday, 13 January 2016



 HERI YA MWAKA MPYA

Ndugu wapendwa wa Kivulini kwetu Blog tunayo furaha kuwafahamisha kuwakaribisha tena kuendelea na maongezi yetu Kivulini baada ya kupoteana kwa muda mrefu kidogo.

Awali ya yote tungependa kuwamwagia salamu nyingi za mwaka mpya wa 2016 tukiwa na inani kuwa mtakuwa hamjambo na mnaendelea vema na shughuli zenu za kila siku.

Kwa kuwa leo tulikuwa tunawaalika tu katika Blog hii tusingependa kuwachosha na maelezo ya nini ilikuwa sababu ya kupoteana; tunadhani mnachokihitaji zaidi ni huduma.

Tutaendelea kupashana na kutaarifiana mwenendo mzima kuhusiana na Blog yetu.

Tnachukua fulsa hii kuwaahidi mema kwa mwaka huu wa 2016. Tunawakaribisha wote.

Asanteni sana.


Tuesday, 7 July 2015

SIMU KUTOKA KWA MGOMBEA MTARAJIWA

Leo alfajiri Kivulini kwetu tumepokea ujumbe wa sauti ufuatao toka kwa Ndugu yetu Mheshimiwa sana mgombea mtarajiwa :

"Halo ndugu zangu Kivulini,

Muda wowote kuanzia sasa Chama chetu kitaanza mchakato wa kutuchuja. Wakati tukisubiri muda huo ufike nilitaka niwatoe hofu wapenzi wangu wote kuwa uwezekano wa mimi kuwemo katika kumi bora hauna shaka kabisa.........tano bora pia sina wasiwasi..............kidooogo nina mashaka na tatu bora; japo hapo napo endapo sifa zitazingatiwa ipasavyo naweza kuvuka.

Moyo wangu unanidunda sana katika kuteuliwa kuwa mgombea pekee wa nafasi hiyo muhimu. 

Kitu kingine ambacho ningependa kuwapa kama akiba ni kuwa mmoja kati ya jamaa zangu endapo nitaingia nae katika tatu bora nina uhakika kabisa na nafasi ya ugombea mwenza.

Baada ya kuwapa matumaini hayo ningelipenda kuwafahamisha kwamba nitakuwa radhi na matokeo yoyote ili mradi rafiki zangu wawili hawatakuwemo katika tano bora. Nasema hivyo kutokana na harakati zao ambazo kwa kiasi kikubwa kiliathiri sana mchakato huu kwa wagombea wengi tangu utangazaji nia, uchukuaji fomu mpaka urejeshaji fomu kiasi kwamba sina imani na hata mienendo yao hapa mjini katika kipindi hiki kigumu cha subra.

Kitu ambacho ninawapasha wana Kivulini kwetu na wapiga kura wote ni kuwa jiandaeni safari hii kushuhudia maajabu katika uteuzi kwani hautakuwa ndani ya matarajio yenu mlio wengi. Matokeo ya uteuzi yatawaacheni midomo wazi. Cha msingi wote mtafurahia uteuzi huo ambao hautarajiwi.

Mimi japo sijitaji ni miongoni mwa hao ambao wapo nje kabisa ya mawazo yenu na nina matumaini makubwa kabisa ya kuwa mgombea mtarajiwa. Hata hao watakaoingia tatu bora mtashangaa na roho zenu.

Ili nisije nikasema na kupitiliza naomba niishie hapa nikiwaomba ndugu na rafiki zangu mniombee niteuliwe kwani mimi ndiye nitakayekuwa mkombozi wenu pekee  miongoni mwa wagombea wote.

Ahsanteni sana kwa kunisikiliza."

Tulidhani ni vizuri tukawaonyesha wote ujumbe huu ambao ni kama utabiri wa aina yake ambao pengine utaweka vizuri kisaikolojia wale ambao kwa muda sasa tumekuwa tukijiapiza kuwa matokeo yatakuwa yale tunayoyawaza sisi.

Friday, 22 May 2015


TUSIENDEKEZE UTAMADUNI WA MIGOMO

Kivulini kwetu kwa kipindi kirefu tulikuwa tumesimama kukutana chini ya mti wetu kutokana na hali ya hewa ya mvua na kwamba chini ya mti wetu kulikuwa na tope na unyevu hivyo tulikuwa tunasubiri hali iwe shwari.

Wakati tukiwa katika subira kuna mambo kadhaa yalitokea ambayo kwa hakika mara hali iliporejea kuwa nzuri tulianza nayo katika mijadala yetu.

Moja ya mambo ambayo tulidhani ni muhimu tukaeleweshana ni suala la migomo.

Ni kweli kuwa nchi yetu ni nchi ya demokrasia tena ya vyama vingi. Ni nchi inayoamini katika utawala bora. Ni nchi inayojali haki za binadamu. Ni nchi ambayo inajitahidi sana katika kukwepa udikteta na kuamini kila mtu kujieleza na kudai haki yake kwa kadri ya uwezo wake; wakati mwingine hata kama haki hiyo haipo; mtu ashindwe mwenyewe.

Haki ya mtu kugoma siyo mjadala mkubwa kwetu; mjadala kwetu ni matokeo ya migomo hiyo na namna migomo hiyo inavyochukuliwa.

Tuchukue mfano walipogoma wafanya biashara kufungua maduka wakilalamikia mashine za kukatia risiti. Kwa kuwa ni watu wazima wenye akili timamu tunaamini kabisa walikuwa wanajua wanachokidai. Lakini walipofunga maduka yao nchi ilikosa makusanyo ya mapato kwa siku zote walizogoma. Mapato hayo kwa hesabu zake lazima yalikuwa makubwa na yangeweza kutupa huduma nyingi sisi wananchi wa nchi hii ambamo  na wao wamo. Hatukuelezwa ni hasara ya kiasi gani ilipatikana, pengine akina sisi tungelikasirika zaidi. Madai ya mgomo huo yalikuwa ni ya muda mrefu na kama yangelijadiliwa na kupatiwa ufumbuzi; ufumbuzi ambao umekuja kupatikana baada ya mgomo; hasara hiyo isingelipatikana.



Hasara nyingine ni ya usumbufu kwa wananchi ambao walikuwa wanahitaji kununua aidha vyakula au vifaa mbalimbali kwa ajili ya kazi zao. Wengine walikuwa wametoka sehemu moja kwenda nyingine kwa ajili ya kufanya manunuzi. Wote hawa mbali na usumbufu wapo walioingia gharama kutokana na maduka hayo kufungwa. Gharama hizo hawana wa kumdai.

Mfano mwingine ni mgomo wa madereva. Hawa waligomea kusomeshwa tena kusomeshwa kwa gharama kubwa waliyodai iko nje ya uwezo wao. Waligomea pia kufanyishwa kazi bila ya mikataba na malipo madogo na mapungufu mengi katika ajira zao. Hili nalo lilikuwa linaweza kuzungumzwa na wahusika na kufikia makubaliano ambayo yalikuja kufikiwa baada ya mgomo. Kilichotokea wakati wa mgomo huo ni usumbufu kwa watu chungu nzima.



Sijagusia mgomo wa wenye magari ya usafirishaji, migomo bubu ya kufunga barabara ambayo sasa hivi imeshamiri; usilogwe sasa hivi kumgonga japo mbwa wa mtu; kesho utakuta mawe yamepangwa barabarani wahusika wakidai hiki ama kile.



Kivulini kwetu tunasema kuwa kila kunapotokea migomo huwa wanaoathirika zaidi ni watu ambao hawahusiki kabisa na chanzo cha migomo hiyo wala hawana maamuzi yoyoye juu ya utoaji wa hayo yanayogomewa. Na pindi wanapopata hasara iwe ya gharama yoyote huwa hawana wa kuwafidia na wakati mwingine huwa hata radhi hawaombwi. Hii kwa kweli si haki. Kama waliogonma walikuwa wakidai stahiki zao; iweje hawa nao walioathirika na migomo bila kuhusika na lolote wawe hawana haki yoyote.



Kivulini kwetu tulikuwa tunaiomba jamii yetu itafakari upya juu ya utaratibu huu wa kudai haki kwa kukiuka haki za wengine. Mwingine kumwaga damu kwa ajili ya kutetea damu ya mwingine bila makubaliano yoyote.

Kivulini kwetu pia tulikuwa tunaiomba jamii ielewe kuwa wasije wakadhani makundi mengine yameridhika na hali zao; kilichopo ni kuwa makundi mengine yanafanya ustaarabu kwa kutiojiingiza katika kero ya kuwakera wengine ili kupata haki zao.

Kivulini kwetu tulikuwa tunawaomba wote waliogoma na wenye nia ya kugoma wakumbuke kuwa endapo kila mtu atagoma kwa wakati wake ili kudai chake, ipo migomo ambayo itagharimu maisha ya wengi. Kumbukeni walipogoma madaktari hali ilikuwaje; kumbukeni walipogoma walimu hali ilikuwaje; kumbukeni walipogoma wanafunzi wavyuo vikuu hali ilikuwaje.


Chukulia Wakulima wakigoma na mazao yao itakuwaje; chukulia Polisi wakigoma kupokea mashtaka yetu tukiparurana uswahilini itakuwaje; Wanajeshi wakigoma kulinda mipaka yetu itakuwaje; Wenye Bar na wauza Bar wakigoma wanywaji itakuwaje, wakigoma wahudumu wa usafi wa majiji wiki nzima itakuwaje mijini; wakigoma wahudumu wa Mochwari mambo yatakuwaje; wakigoma wauza bidhaa masokoni mapochopocho tutayanunua kwa nani; akina mama wakiwagomea waume zao au waume kuwagomea wake zao; hali itakuwaje katika familia zetu; Mahakimu wakigoma wahalifu mtawashitaki kwa nani; Kivulini kwetu tunasema na Rais wetu nae akigoma kama alivyofanya wa Burundi hali itakuwaje...........ebu tubadili huu utaratibu wa kugoma na kusababisha maafa kwa ambao hawakuyasababisha matatizo yetu. Tuwe na utaratibu wa kuzungumza na kukubaliana mapema; hii ni kwa wanaodai na wanaodaiwa; kama uwezekano upo basi wenye haki yao wapewe mapema kuliko kusubiri mpaka wengine wasumbuliwe ndipo mje na kukubali mnachoombwa.



Kivulini kwetu tunaamini kwamba ni wajibu wetu kuelimishana na kuwekana sawa kwa sababu kila mtu anayo haki yake kama aliyonayo mwenzake. Kuwepo na utulivu haina maana ya wasiogoma kuridhika na kila kitu bali ni ustaarabu wa kuamia kutumia busara katika watu kupata mahitaji yao na kudsai haki zao bila ya kuwasababishia wengine usumbufu vinginevyo kila mtu akiingia mtaani kudai chake hatutakuwa na nchi kama ilivyo sasa bali uwanja wa mauti.

Sunday, 5 April 2015

TABIA MBAYA ZA WAHUDUMU WA BAR NA HOTELI

Kama mjuavyo leo ni sikukuu ya Pasaka. Pamoja na kuwa si maadili lakini hiyo ndiyo hali halisi ilivyokuwa; Kivulini kwetu na sisi tuliamua kutoka kwenda maeneo kusafisha macho. Hatukwenda wote sehemu moja bali tulitawanyika maeneo mbalimbali kwa maelekezo kwamba ifikapo muda tuwe tumerejea kujumuika pamoja kama familia kupata kilichoandaliwa kwa ajili ya siku ya leo.

Kivulini kwetu kutokana na utaratibu wa kuongozwa na nidhamu, ulipotimu muda kila mmoja wetu alifika nyumbani mapema. Kwa kuwa tulikuwa tumewahi ilibidi kusubiri kidogo maandalizi yakae sawa tupate kuendelea na kipindi hicho. Wakati tukisubiri ilianzishwa mada ambayo kutokana na umuhimu wake tusingelipenda kuwanyima ndugu zetu uhondo; na pengine kupata maoni juu ya namna ya kukomesha tabia hizi za hawa ndugu zetu wahudumu.

 Image result for wahudumu wa bar



Mmoja wetu kutokana na alichokiona alisema wahudumu hawa na hasa wa kike wana tabia mbaya sana ya kuwaombaomba wateja wawanunulie soda, bia ama chakula. Inasemekana huwa nawaoni haya wala vibaya kumwomba mteja hata kama hiyo ni mara ya kwanza wameonana nae. Kwa namna wanavyoomba humfanya mteja akereke kiasi kwamba hata akimpa huwa anampa kwa shingo upande ili kuondoa hiyo kero ili aendelee na starehe zake bila ya bugudha yoyote.

 Image result for wahudumu wa bar

Kituko kingine cha hawa wahudumu ni uzito wa kurejesha chenji na hata wakirejesha huwa siyo kamili kwa kisingizio cha chenji kuwa tatizo. Penye 800/= ukitoa noti ya sh. 1000/= usitarajie kuipata 200/=; penye 4000/= au 4500/= ukitoa noti ya sh. 5000/= usutarajie kuipata sh. 1000/= au 500/= na ukiipata ni sharti ugombane. Hii ni kwa upande wa chenji; lakini pia kuna mchezo wa kuongezeana bei; chakula cha 2500/= utatajiwa sh. 3500/=, ama chakula cha 4000/= utaambiwa sh. 4500/= au 5000/= ili mradi kipatikane kiasi chochote mbali na kiasi stahiki wakichukue kama chao. Kazi kubwa huwapata wale ambao huwa wamelewa kidogo ama wanaoonekana wana pesa nyingi na hawapendi kulumbana au kuonyesha wana gubu kwa kudaidai chenji.

Tatizo jingine lililobainishwa kwa ndugu hawa ni udoezi. Wapo wahudumu hasa akina dada ambao hudiriki kwenda kunawa maji kabisa na kuja kuketi mezani kwa wateja na kuanza kula nao vipande vya kuku na mishikaki bila ya hata kukaribishwa kwa kisingizio cha kuonja kama vimeiva au chumvi imekolea; pengine husingizia kuwasindikiza wateja kimaongezi. Wapo ambao huchukua glasi na kumimina soda ya mteja au bia na kunywa. Ukiwaona unaweza kudhani ni wacheshi kwa wateja kumbe ni wadoezi wakubwa.

Tuliambiwa kwamba wapo wahudumu visirani ambao hupenda kuwahudumia wateja wanaokuja peke yao tu na pindi wajapo na wenza wao huwa ni wazito kutoa huduma na watoapo huwa wanenuna ama hutoa huduma mbaya kwa makusudi. Ukiagiza bia baridi utaletewa ya moto, ukiagiza supu ya kuku utaletewa ya mbuzi na wakati mwingine unaweza kuambia kitu fulani hakipo kumbe kipo; wao huwa ni vituko kwa kwenda mbele ili mradi siku nyingine usirudie tena kuja sehemu hiyo na huyo uliyeongozana naye.

Wapo wahudumu ambao wakikuzoea sana huwa hawana adabu wala heshima; anaweza kusema chochote na popote bila kujali uko katika mazingira gani ama uko na nani. Aweza kukwambia amekumiss sana wakati hana uhusiano na wewe; aweza kuanza kukuuliza hali ya mkeo au mmeo wakati hamjui; aweza kukucheka kuwa umefulia kwa sababu leo unakunywa soda badala ya bia; anaweza kukwita shemeji kwa sababu tu jana alikuona umekaa na rafiki yake. Wabaya zaidi ni wale ambao hupita wakitangaza kuwa mteja fulani ni mtu wake na kutoa onyo kwa wenzie wasimhudumie isipokuwa yeye; na wakati mwingine hutwangana makonde kumgombania mtu ambaye hana habari nao kabisa; kisa ni kuwa mteja anaonekana anazo. Utashangaa kama una mazoea na sehemu siku unakwenda unaona kila mhudumu anaogopa kukusogelea kutokana na vitisho wakati mteja mhusika hujui kinachoendelea.

Kero jingine ni wahudumu  ambao huja kazini na kutumia muda wao mwingi kuchezea simu na kusoma magazeti ama kuongea na washikaji wao na kuacha kuwahudumia wateja. Mteja anaweza kukaa zaidi ya dakika kumi bila ya kuulizwa ahudumuwe nini na wakati huohuo kuna wahudumu kibao wamezagaa na kila mmoja anafanya lake ambalo ni nje ya majukumu yake ya kazi. Na akitokea mteja kujaribu kulalamika; majibu atakayopata hatodiriki kurejea tena mahali pale.

Kivulini kwetu baada ya kupata aina hizi za wahudumu tulijaribu kujiuliza kuwa ni nini chanzo cha matatizo hayo. Tulichogundua ni sababu kadhaa ambazo tunadhani zikifanyiwa kazi matatizo haya ya huduma za hoteli na bar yatapungua kama siyo kwisha kabisa.

Tulibaini kuwa sababu ya kwanza ni kuwa wahudumu wengi hawakusomea kazi hizo na wala kupigwa japo msasa wakati wanapatiwa ajira hizo hivyo hawana kabisa elimu yoyote juu ya wanachotakiwa kukifanya; na kuna wengine ambao huwa hata darasa la saba hawakumaliza. Tunadhani wakati umefika wa wenye mahoteli na bar kuajiri wahudumu waliopitia mafunzo ili huduma zikidorora tujue ni sababu nyingine na si ya elimu au mafunzo.

Tulibaini pia kuwa hawa wahudumu wengi hulipwa mshahara mdogo sana usiotosheleza hata nauli ya kuja kazini kwa wiki mbili na pamoja na kuwa mshahara ni mdogo huwa hawapewi wote kwa pamoja na bado kiasi kikubwa hukatwa kwa kisingizio cha kuvunja chupa, glasi n.k. ama kupata shoti katika malipo ya huduma; hivyo ili waweze kumudu maisha inabidi wawe ombaomba kwa wateja wao kufidia upotevu ama kupata cha kurudi nacho nyumbani kwa matumizi yao. Wengine inasemekana hupatiwa nafasi ya kuhudumia lakini bure kwa makubaliano kuwa atumie uwepo wake mahali hapo kupata pesa ya kujikimu; vipi atapata hiyo huwa ni akili kichwani mwake. Tunadhani waajiri wa wahudumu hawa wawe waungwana kwa kuwalipa kwa mujibu wa sheria na kanuni kwani maisha ni magumu na hali ni ngumu sana ya maisha; kumtumikisha mtu bila ya kumlipa sio uungwana hata kidogo.

Tuligundua pia kuwa wahudumu hawa huajiriwa kwa kufuata sura zao na maumbile yao kuwavutia wateja na wala si uwezo wao wa kazi ama wito wa kazi. Na mbaya zaidi hulazimika kutoa rushwa ya ngono kwa wamiliki wa mahoteli ama mameneja wahoteli na bar hizo. Hivyo huwa na kiburi toka siku ya kwanza kwa kuamini hata akifanya madudu tayari alikwisha hakikishiwa usalama wa ajira yake na mwenye mali au meneja. Wenye hoteli na bar wakumbuke hawa ni wahudumu wa watu na wanastahili kuheshimu na kuheshimiwa; kuajiri mtu kama kitu ni kuleta kero mahali pa kazi na mwisho wa siku hata biashara hudumaa kutokana na wateja kuacha kuja mahali hapo.

Kitu kingine tulichokibaini ni kuwa wahudumu hawa wengi wao wamepambana na misukosuko ya maisha mapema kabla ya umri wao. Wapo waliopewa mimba na kukimbiwa; kati yao wapo waliozaa na wengine kutoa mimba. Wapo waliofukuzwa au kutengwa na familia zao kwa sababu mbalimbali . Wapo waliokimbia ndoa zao. Wapo waliokimbia masomo n.k. Kutokana na sababu hizo wengi wao wana hasira na maisha na wanatembea na nadhiri kuwa siku wakipata mwanya wakufanya lolote kulipiza kisasi wanaweza kufanya. Wanaweza kumwibia tajiri, wanaweza kumuibia mteja, wanaweza kumchoma mtu kisu n.k. Hali hii hufanya maeneo ya hoteli na bar kuwa kichaka cha kuficha kundi la watu wenye hasira na walipa visasi ambao kila mtu mbele yao humwona adui. Matajiri wawe makini katika kuajiri kwa kujaribu japo kupata historia za wafanyakazi wao ili kuwa na uhakika wa usalama mahala pao pa kazi.

Kuvilini kwetu inaamini sana katika huduma bora kwa mteja na haki kwa wafanyakazi; na ili kwenda sawa ni vema kufuata taratibu na sheria katika ajira za wahudumu.